20 September 2013

WANASIASA WAJIBU MAPIGO YA KIKWETE


  • KUNDECHA ATANGAZA KUJIUNGA NA WAPINZANI
 Na Mariam Mziwanda
Viongozi wa vyama vilivyoingia ushirikiano vya CHADEMA, CUF na NCCR -Mageuzi, wamesema, mchakato wa kupata katiba mpya lazima ufanyike kwa maridhiano, vinginevyo vitisho, dharau na kupuuza baadhi ya maoni hakutasaidia kupatikana kwa mwafaka.

Viongozi wa vyama hivyo wametoa kauli hiyo ikiwa ni siku moja baada ya Rais Jakaya Kikwete, kuelezea kushangazwa na uongo wa baadhi ya wanasiasa hasa madai kwamba aliteua wajumbe wa Tume ya Katiba bila kuongozwa na mapendekezo ya wadau mbalimbali waliopendekeza majina hayo.
Wakizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana viongozi hao ambao ni Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, Mwenyekiti wa CUF, Prof. Ibrahim Lipumba na Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia, alisema mchakato huo unahitaji maridhiano.
Mbowe alisema ikiwa Rais atachukulia kwa mzaha suala hilo na kuamua kusaini mswada huo bila kutafakari kwa mapana yake nchi itaingia kwenye machafuko.“Tunarudia kumshauri na kumsihi Rais Kikwete kwamba katiba ni haki ya Watanzania wote, hivyo inahitaji busara, ushirikiano, uvumilivu, staa, kuangalia maslahi, kuaminiana na vitu vingine kama hivyo,” alisema Mbowe na kuongeza:
“Kamwe hatuwezi kupiga magoti kwa kuomba katiba mpya, katiba sio zawadi kwa wanasiasa na hatupiganii kupatikana kwa katiba nzuri kwa maslahi yetu wenyewe, bali kwa maslahi ya Watanzania wote.”Kwa upande wake Profesa Lipumba, alisema Rais Kikwete ameanza kuonesha dharau kwa mambo yenye maslahi makubwa kwa taifa.
“Kwanza naomba niseme kwamba Rais Kikwete ndiye hajaeleza ukweli kwa Watanzania wanaoishi California, nchini Marekani,” alisema.Naye Mbatia alisema kama Rais Kikwete anadai ametumia mapendekezo ya wadau kuteua wajumbe, anapaswa kuweka wazi anayewakilisha kundi la walemavu.
Mbatia alisema Shirikisho la Watu Wenye Ulemavu Tanzania (SHIVYAWATA) lilipendekeza majina matatu ili achaguliwe mmojawapo, lakini wote walitupwa nje na kufanya kundi hilo kujiona halina umuhimu ndani ya jamii.“Kama kweli anajua ameongozwa na mapendekezo hayo atueleze kila kundi limewakilishwa na nani, yapo mambo mengi tunayolalamikiwa tunataka haki itendeke kwa kila Mtanzania,” alisema.
Kwa upande wa Amiri Mkuu wa Baraza Kuu la Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania, Mussa Yusuph Kundecha, alisema wameungana na upinzani kudai katiba inayokidhi matakwa ya Watanzania.“Tumejadiliana na kuafikiana kuungana ili katiba ipatikane yenye mawazo ya makundi yote, kwa bahati nzuri malalamiko yetu waislamu yamekuwa na uwiano sawa na malalamiko ya wapinzani.
“Sasa kama wote tumekutana na wazo au shida moja lazima tuamue tufanye nini ili tupate jibu, sasa tunataka mswada urudi bungeni ujadiliwe upya ili kuondoa upungufu uliopo na vipengele vilichomekwa kinyemela.”

No comments:

Post a Comment