23 September 2013

WAFANYAKAZI TANAPA WADAIWA KUHUSIKA KWENYE UJANGILI



Na Said Njuki, Arusha

  Wakati ujangili wa meno ya tembo na faru ukiinyima usingizi Serikali, Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA) limewashtukia baadhi ya watumishi wake kutokana na kujihusisha na mtandao wa ujangili kwa kushirikiana na baadhi ya watendaji wa vyombo mbalimbali vya dola.

Kutokana na hali hiyo TANAPA inakusudia kubadili mfumo wake wa kiutendaji kutoka wa kiraia na kuwa mfumo kamili wa kijeshi kwa watumishi wote ili kujiimarisha katika kukabiliana na janga la ujangili nchini.

Meneja Uhusiano wa TANAPA, Pascal Shelutete, aliwaambia waandishi wa habari jana mjini hapa kuwa Serikali haiwezi kuona maliasili ambazo ni urithi wa Watanzania na dunia kwa ujumla, zikiteketezwa na majangili na kuikosesha mapato Serikali.

  Alisema lazima juhudi za makusudi zichukuliwe licha ya majangili hao kuwa na mtandao. Alisema ujangili hasa wa meno ya tembo na faru ni mtandao wa kimataifa unaohusisha watu wa kada mbalimbali, huku majangili hao wakitumia fedha nyingi na vifaa vya kisasa zikiwemo silaha za kivita, hali inayokwamisha jitihada za Serikali za kupambana na uhalifu huo.

  Shelutete alisema Shirika kwa kutumia vyombo vyake vya kiintelejensia vinawachunguza baadhi ya watumishi wake wanaojihusisha na mtandao huo na watakapogundulika na kujiridhisha watachukuliwa hatua kali za kisheria.

  "Shirika linaendelea kuchunguza na kuchukua hatua mbalimbali za kinidhamu na kisheria kwa wafanyakazi wanaobainika kujihusisha na vitendo vya ujangili kwa kushirikiana na vyombo vya dola...uchunguzi unaendelea kufanyika kwa baadhi ya wafanyakazi na ushahidi wa kisheria utakapokamilika kwa wanaojihusisha na mtandao huo hatua za kisheria zitachukuliwa," alisema Shelutete

  "Tumepokea tuhuma dhidi ya baadhi ya watumishi wetu kujihusisha na ujangili, huo ni mwanzo mzuri kwetu katika kuchunguza tuhuma hizo kwa kutumia vyombo mbalimbali... hatukatai kuwa Shirika linaweza kuwa na watumishi wa aina hiyo, bali uchunguzi wa kina utafanyika ili tusimwonee mtu," alisema.

   Alisema shirika linajua ukubwa wa tatizo, hivyo linajiandaa kwa mikakati mbalimbali ili kukabiliana na ujangili na tayari uimarishaji wa doria za magari, miguu na matumizi ya mbwa hifadhini kote nchini hali inayodhihirisha kupunguza kwa kiwango cha vitendo hivyo.

  Alitoa mfano wa hifadhi za Tarangire na Ziwa Manyara akieleza kuwa katika kipindi cha miezi sita iliyopita ujangili ulikuwa umeshika kasi umedhibitiwa kwa asilimia 100 kwa maana hakuna tembo hata mmoja aliyeuawa.

  Alitaja mikakati mingine kuwa ni pamoja na kuanzishwa kwa kikosi maalumu cha kupambana na ujangili na matukio ya dharura, kutoa mafunzo maalumu ya awali kwa askari 100 ambao wataingia katika mafunzo ya awamu ya pili hivi karibuni.

  Aliyataja baadhi ya mafanikio kuwa ni pamoja na kunasa majangili 1,116 ndani ya hifadhi za taifa nchini, wakiwemo majangili 248 walioshikwa Hifadhi ya Taifa ya Serengeti pekee katika kipindi cha Aprili hadi Juni mwaka huu, kukamata silaha za moto 85 na waya zinazotumika kutega wanyama 25,422, mbao 3,275' mbao 1030 na mifugo 6,650.

No comments:

Post a Comment