19 September 2013

MSWADA WA KATIBA SASA KAA LA MOTO



Na Goodluck Hongo
MSWADA wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba umezidi kugeuka kaa la moto kutokana na kuongezeka kwa shinikizo kutoka kwa watu na taasisi mbalimbali wanaomtaka Rais Jakaya Kikwete, asisaini mswada huo ili kuwa sheria kwa kile kinachodaiwa kuwa ulipitishwa kiujanjaujanja.

 Ili kuhakikisha muswada huo hausainiwi, vyama vitatu vilivyoungana kupinga mchakato wa Katiba Mpya vya CHADEMA, NCCR-Mageuzi na CUF vimezidi kutafuta nguvu ya kuungwa mkono kwa kukutana na makundi mbalimbali ndani ya jamii kwa lengo la kuunganisha sauti ili kukwamisha mswada huo. 
Jana, viongozi wa vyama hivyo, Freeman Mbowe (CHADEMA), Prof. Ibrahim Lipumba (CUF) na James Mbatia (NCCR-Mageuzi) walikutana na viongozi wa Shirikisho la Vyama vya Watu Wenye Ulemavu Tanzania (SHIVIWATA) na kuwaeleza kasoro zilizoko kwenye mswada huo kwa lengo la kutaka kuungwa mkono.
Mazungumzo ya viongozi hao na SHIVIWATA yalifanyika jana asubuhi na baada ya kumalizika wanasiasa hao waliendelea na ratiba yao ya kukutana na vyama vingine vya walemavu vidogo vidogo Makao Makuu ya CUF, Buguruni, jijini Dar es Salaam.
Mikutano hiyo ya vyama hivyo vitatu vya siasa ni mwendelezo wa mikutano mingine ambayo tayari imeishafanyika tangu wabunge wake wasusie mjadala wa Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Katiba Mpya.
Tangu kumalizika kwa Bunge, vyama hivyo vimeshafanya mikutano na Jukwaa la Wahariri Tanzania, Jukwaa la Katiba na SHIVIWATA; na Jumamosi vitafanya mkutano mkubwa viwanja vya Jangwani ili kueleza jinsi mswada huo ulivyopitishwa kiujanja ujanja.
Wakati hayo yakiendelea wadau mbalimbali wameshauri mswada huo usithubutu kupelekwa Ikulu kwa Rais Kikwete ili ukasainiwe na kuwa sheria.Wakizungumza Dar es Salaam jana wakati wa mjadala wa wazi wa nini kifanyike hadi sasa mchakato wa mabadiliko ya katiba ulipofikia, wadau hao walisema yanatakiwa yafanyike maombi ya kukwamisha mswada huo.
Mjadala huo ulioandaliwa na mtandao wa jinsia (TGNP). Mwenyekiti wa Jukwaa la katiba, Deus Kibamba, alisema mchakato wa mabadiliko ya Katiba haukuanza kwa huruma ya Rais Kikwete, bali watu waliudai kwa zaidi ya miaka 20 iliyopita, hivyo inabidi ufanyike kwa uwazi.
Alisema huo ni mchakato wa kwanza kufanyika kwa wananchi kutoa maoni yao, lakini umeanza kutushinda kutokana na wananchi kukosa elimu ya katiba.Aliyekuwa Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dkt. Xavery Rweitama, alisema mjadala wa mswada huo umetekwa na wanasiasa jambo ambalo limekuwa mwiba mkali kwao.
Alisema kuna wanasiasa wa ajira na wale ambao wanataka masilahi ya wananchi. Alisema Tume ya Mabadiliko ya Katiba imetokana na shinikizo la nje ya bunge ndiyo maana imeweza kufanya mambo mazuri ikiwa ni pamoja na kupendekeza Serikali tatu.Alisema suala la Serikali tatu limekuwa mwiba mkubwa kwa CCM kutokana na chama hicho kuamini kuwa kinaweza kutawala milele.
Naye Mwakilishi Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) Anna Henga, alisema kwa sasa kuna hali ya wanasiasa kuteka machakato wa katiba kwani wananchi wamebaki kuzungumzia Serikali tatu tu.Alisema ni lazima wananchi wajue kutenganisha siasa na Katiba Mpya, kwani walio wengi wanaamini kuwa wahusika wakuu ni wanasiasa na si wananchi.

1 comment:

  1. Kaa la moto kwa nani? Mnajidanganya kama sio wasomi? Upinzani hauna uwezo wa kuzuia mswada wowote kama demokrasia inatumika bungeni. Wasomi wanaelewa hivyo. Wasaidieni upinzani kupata majority bungeni kwa njia halali ili waingize agenda zao wanazotaka. Kwa sasa haiwezekani kama kweli bunge linaendeshwa kwa utashi wa kidemkrasia na kupiga kura.

    Pia muelewe wananchi wa kawaida hawaelewi hoja mnazopigania! wanshabikia tu kwamba "Sugu bwana kampiga ngumi askari" basi. Msitegemee nguvu ya umma kumng'oa JK mnaota ndoto za mchana

    Jk anapendwa na wananchi wengi wa kawaida. Anafanya kazi kwa uangalifu sana wala sio kwa jazba!

    ReplyDelete