03 September 2013

DEMOKRASIA YA KWELI MSINGI WA AMANI, UTULIVU



 Na Suleiman Abeid
 MWAKA 1992, ni mwaka muhimu kwa Watanzania kufuatia mabadiliko makubwa ya mfumo wa siasa yaliyofanyika ambapo taifa letu lilitoka katika mfumo wa utawala wa chama kimoja na kuanza kutumika kwa mfumo wa vyama vingi.

Pamoja na kukubalika kwa mfumo huo nchini kulitokana na busara za uongozi uliokuwepo madarakani wakati huo kuchukua maamuzi mazito ambayo wananchi wengi hawakuyategemea.Maamuzi hayo ni kitendo cha Taifa kukubali kuingia katika mfumo wa vyama vingi wakati wananchi wake waliukataa mfumo huo kupitia Tume maalumu iliyokuwa imeundwa kukusanya maoni ili kuweza kubaini iwapo nchi iingie katika mfumo huo au ibaki katika mfumo wa chama kimoja.
Kwa mujibu wa matokeo yaliyotangazwa na tume iliyokuwa ikikusanya maoni hayo, asilimia 80 ya Watanzania waligoma Tanzania kuingia katika mfumo wa vyama vingi, huku hoja ya msingi ya kuukataa mfumo huo ikiwa ni kuchelea kutokea mapigano ya wenyewe kwa wenyewe.Busara za Baba wa Taifa, hayati Mwalimu Julius Nyerere zilisaidia aliposhauri kwamba, pamoja na Watanzania wengi kuukataa mfumo huo ilikuwa vyema mawazo ya Watanzania asilimia 20 waliokuwa wamekubali kuanzishwa kwa mfumo huo yakaheshimiwa na kuchukuliwa.
Kutokana na ushauri huo, hatimaye mwaka 1992, ilikubali kubadili katiba yake na kikubwa katika mabadiliko hayo ilikuwa ni kubadilisha kifungu cha katiba kilichokuwa kikieleza kwamba, Tanzania itakuwa nchi ya chama kimoja na badala yake ikawa, "Tanzania itakuwa ni nchi ya mfumo wa vyama vingi".
Mfumo wa vyama vingi ni hali ya kuwa na chama zaidi ya kimoja, katika nchi moja kwa lengo la kuleta ushindani wa kisiasa, ili kuleta maendeleo ya nchi.
Upinzani wa kisiasa si uadui kama asilimia 80 ya Watanzania waliokuwa wameukataa mfumo huo walivyokuwa wakiamini.Ukweli ni kwamba nchi yoyote ulimwenguni yenye demokrasia ya kweli inatumia mfumo wa vyama vingi vya siasa kwa lengo la kuongeza wigo wa demokrasia kwa wananchi wake ambapo chini ya mfumo wa chama kimoja sehemu kubwa ya wasio wanachama wa chama tawala hawakuwa na eneo la kuchangia mawazo yao katika kuongoza nchi.
Kuanzishwa kwa mfumo huo, kulifungua milango ya kuanzishwa kwa vyama vipya vya siasa mbali ya kile kilichokuwepo Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambapo vyama vya awali vilivyoanzishwa ni pamoja na Chama cha Wananchi (CUF).Vingine vilikuwa, Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Demokrasia Makini, Democratic Party (DP), National Convention for Constitution and Reconstruction-Mageuzi (NCCR-Mageuzi), United Democratic Party (UDP), UMD na vingine.
Mpaka kufikia mwishoni mwa mwaka 2011, zaidi ya vyama vya siasa 18 vilikuwa vimeanzishwa nchini, vyote vikiwa na lengo kuu moja la kupanua demokrasia katika suala zima la utawala wa nchi na pia kuweza kupata ridhaa ya kuongoza nchi ambapo kwa kawaida ni chama kimoja tu ndicho hupata ridhaa hiyo.
Chama ambacho hakikufanikiwa kupata ridhaa ya kukamata dola na kuunda serikali, lakini kikapata idadi kubwa ya wabunge wanaoingia katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kinapokuwa ndani ya bunge hupewa heshima ya kuongoza kambi ya upinzani kwa maana nyingine hujulikana kama chama kikuu cha upinzani.
Upinzani hapa maana yake si kuwa na chama kinachoongoza mapambano yanayolenga kuifanya nchi isitawalike la hasha, maana halisi ni kule kukosoa muswada ama sheria yoyote ile inayopelekwa bungeni ikiwa haina masilahi kwa wananchi.
Kutokana na hali hiyo kambi ya upinzani hupinga mswada au sheria hiyo kwa maslahi ya watanzania ambapo pia hupaswa kutoa ushauri wa njia mbadala itumike kwa lengo la kuleta maslahi bora zaidi kwa wananchi.
Ipo mifano mingi juu ya hili mmojawapo ni wa mabadiliko ya sheria ya ukusanyaji maoni Katiba Mpya.
Kwa wanaoamini kwamba, uwepo wa vyama vingi nchini ni kwa ajili ya kuleta machafuko, ni wazi wamefilisika kifikra, wanapaswa kufuta mawazo hayo na kurejea katika mistari kwa kuviona vyama vya upinzani vipo kwa ajili ya kukionesha njia ama kukikosoa chama tawala kilichoko madarakani pale kinapokwenda kinyume na malengo ya nchi.
Iwa p o c h ama k i l i c h o p o madarakani kitakaa tu katika kiti chake cha enzi na kukosa mtu wa kukikosoa; ni wazi kwamba utawala wake utakuwa ni wa ki-imla na wananchi wanaoongozwa na chama hicho watakuwa wako kifungoni daima kutokana na chama kujisahau kwamba kilichaguliwa ili kiwatumikie wao.
Kutokana na hali hiyo kila Mtanzania ana wajibu sasa wa kuviona vyama vyote vya siasa hapa nchini vina haki sawa na tofauti yao ni kwamba, kimoja kati yao ndicho kinachokuwa kimepewa ridhaa ya kuongoza nchi baada ya kunadi sera na ilani yake kwa wapigakura na pale waliporidhika wakakipatia ridhaa hiyo ya kukamata dola na kuunda serikali.
Daima tunapaswa kuelewa kuwa vyama vya siasa ambavyo havikupata ridhaa ya kukamata dola na kuunda serikali si adui au vina lengo la kutaka kuleta machafuko nchini la hasha bali ni kwamba ili demokrasia ya vyama vingi vya siasa iweze kuwa na maana ni muhimu nchi ikawa katika hali ya amani na utulivu wakati wote.
Ili hali ya amani na utulivu iweze kupatikana daima suala la kuvumiliana kati ya wafuasi wa vyama ni lazima lipewe kipaumbele, hasa kwa vyama vile vilivyofanikiwa kupata wabunge wanaoingia bungeni kwa kujenga utamaduni wa kukosoana bila ya kupigana au kuzomeana.
Katika hili chama tawala ndicho kinachopaswa kuwa mfano kwa kuelewa ipo siku moja kitajikuta kimekaa katika viti vya upande wa upinzani na kilichokuwa chama cha upinzani ndicho kimekuwa chama tawala, hivyo kisipoonesha mfano mzuri; ipo hatari ya kulipizana visasi ambavyo vinaweza kuwa chanzo cha kupotea kwa hali ya amani na utulivu nchini.
Ha t a h i v y o , p amo j a n a matatizo yaliyowahi kujitokeza nchini na kuhusisha vyama vya upinzania ikiwa sasa imetimia miaka 21 tangu kuanzishwa kwa mfumo huu, Watanzania wengi wameanza kuielewa vyema dhana ya demokrasia ya vyama vingi ikilinganishwa na pale mwanzo.
Uelewa wa Watanzania utasaidia sana kuifanya nchi kuendelea kuwa ya amani na utulivu na hata kasi ya kuongezeka kwa uchumi itakuwepo iwapo chama tawala kitasimamia katika kuongoza kwa haki na kuwatumikia wananchi waliokiweka madarakani badala ya kujali masilahi binafsi, maana haki ndiyo msingi mwingine wa amani.
Mara kwa mara CCM imekuwa ikikiri maneno ya hayati wa Baba wa Taifa, aliyowahi kusema enzi ya uhai wake kwamba, “pasipokuwa na haki hapawezi kuwa na amani,” Kauli hii ni sahihi maana Tanzania kwa kiasi kikubwa imefanikiwa kuwa nchi yenye amani na utulivu kutokana na sera zake zinazoweka mbele uhuru, haki, usawa na utu.
Msingi huu uhakikishe hauvunjiki daima hata kama CCM itaondoka madarakani na kuwepo kwa chama kingine cha siasa, ili amani iweze kuendelea kudumu hapa nchini ni muhimu kuheshimiana na kuvumiliana.
Kuvumiliana katika suala la siasa ni kitu muhimu, Tanzania ni yetu sote, hivyo si vyema kwa wanachama wa CCM kujiona bora kuliko wale wa vyama vingine, au wale wa vyama vingine kujiona wao ndiyo wanaojua zaidi ya wale wa CCM na kila jambo kinachofanya ni baya.
Utamaduni wa kudharauliana ukipewa nafasi ni wazi tutafika sehemu nchi haitatawalika kabisa na hivyo amani na utulivu uliopo hivi sasa vitatoweka kwa kasi ya ajabu baada ya kundi moja kushindwa kuvumilia manyanyaso na vitendo vya haki za wananchi kukandamizwa kwa makusudi.
Hivyo kila Mtanzania anapaswa kurejea katika katiba iliyopo sasa ambayo inatamka wazi kwamba, Tanzania itakuwa ni nchi ya mfumo wa vyama vingi vya siasa hivyo ili kifungu hicho kitumike vyema ni vizuri demokrasia ya kuvumiliana ikapewa uhuru ili kuendelea kuilinda amani iliyopo nchini.

.





1 comment:

  1. SINA UHAKIKA DEMOKRASIA INAYOHAMASISHWA NA NCHI ZA MAGHARIBI NIYA KWELI AU UNAFIKI KWA KUWA UWEZO WA KUFIKIRI WA WAAFRIKA UKO CHINI NDIO SABABU RAIS OBAMA ALIPOFIKA SENEGALI ALIWAAMBIA KUWA DEMOKRASIA KAMILI NI ILE INAYORUHUSU NDOA YA JINSIA MOJA NI VEMA WAAFRIKA TUKAJIANDAA NA JUHUDI ZA DUNIA KUHUSU"MPANGO MPYA WA ULIMWENGUNI WENYE NIA YA KUSUKA ULIMWENGU UPYA ILI UWEZE KUWA TOFAUTI NA WA SASA KIUCHUMI,KISIASA NA KIJAMII KULIKO KUPAMBANA NA MBUZI WA KUCHONGA"

    ReplyDelete