28 August 2013

YANGA YAILALAMIKIA TFF ADHABU YA NGASSA



 Na Amina Athumani
UONGOZI wa Yanga umelalamikia rufaa waliyoiwasilisha Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kupitia Kamati ya Sheria na Hadhi za wachezaji kuhusu kupinga kufungiwa mchezaji wao, Mrisho Ngassa bado haijasikilizwa huku muda ukizidi kwenda.

Akizungumza Dar es Salaam jana, Katibu Mkuu wa Yanga, Lawrence Mwalusako alisema waliwasilisha rufaa hiyo tangu Agosti 23, mwaka huu, lakini hadi jana haijasikilizwa na endapo watashindwa kupewa ufafanuzi kuhusu pingamizi hilo, watafuata hatua na taratibu stahiki.
Alisema rufaa waliyoiwasilisha ni kupinga adhabu aliyopewa Ngassa, ambayo wanadai ni ya uonevu na inakiuka kanuni za mashindano, misingi ya sheria na haki za msingi za mchezaji wao.
Alisema Yanga ilipokea barua ya TFF Agosti 16, mwaka huu ikielezea adhabu aliyopewa Ngassa ya kufungiwa mechi sita na adhabu ya kulipa faini ya sh. milioni 30 na riba ya asilimia 50 ya sh. milioni 15 ambazo zinafikia jumla ya sh. milioni 45, huku wakishindwa kutaja kifungu cha kanuni aliyokiuka mchezaji wao.
"Yanga inaiona adhabu hii kuwa ni ya uonevu, kwa klabu na mchezaji inayokiuka kanuni za mashindano hayo, misingi ya sheria na haki za msingi za mlalamikiwa," alisema Mwalusako.Alisema sababu za Yanga kuwasilisha rufaa yao na kupinga adhabu hiyo TFF ni kamati kukosea kanuni na sheria ya kumuadhibu Ngassa kwa kuzingatia mkataba batili uliowasilishwa na Simba.
"Suala la usajili wa mchezaji Ngassa, baina yake na Simba mara baada ya msimu wa 2012/2013 kumalizika ulikuwa na matukio makubwa yaliyomhusu Ngassa, Klabu ya Simba na Klabu ya Azam."Kamati ya sheria na hadhi za wachezaji ya TFF ilipaswa kuyarejea, kabla ya kufikia uamuzi waliofikia hasa kwa kuzingatia mchezaji hakuwepo kujitetea katika kikao hicho," alisema Mwalusako.
Alisema pia kamati ilikosea kanuni na sheria kwa kutoa uamuzi kwa ushahidi wa upande mmoja pasipo kumsikiliza Ngassa, pia ilikosea kumuadhibu kwa kuingia mkataba na Simba nje ya kanuni za usajili.Mwalusako alisema pia pingamizi hilo linaeleza kuwa kamati hiyo, ilikosea kisheria kwa walioweka pingamizi kuwa sehemu ya kutoa uamuzi ambapo pia ilikosea kikanuni kuinyima Yanga kumtumia, Ngassa katika mechi sita pasipo na sababu za msingi.
Alisema kutokana na sababu hizo anaimani rufaa yao, itasikilizwa na kutendwa haki inayostahiki kwa mchezaji wao, ikiwa ni pamoja na kumuondolea adhabu ambazo hakustahili mchezaji wao kupewa.Ngassa mpaka leo atakuwa amekosa mechi tatu, kati ya sita zilizomo katika adhabu yake ikiwa ni mechi ya Ngao ya Jamii dhidi ya Azam, Ashanti United na Coastal Union inayotarajiwa kuchezwa leo.

No comments:

Post a Comment