20 August 2013

WATUHUMIWA KUIBA TERANSFOMA



Leah Daudi na Flora Nkya
JESHI la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, linawashikilia watuhumiwa wawili, mmoja kati yao ni dereva wa gari la Shirika la Umeme nchini (TANESCO), kwa tuhuma za kuiba transfoma ambayo ni mali ya shirika hilo.

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Kamanda wa Polisi wa kanda hiyo, Kamishna Suleimani Kova, alisema washtakiwa hao walikamatwa Agosti 16 mwaka huu, saa 6:30 usiku huko, eneo la Ofisi za TanescoKinondoni.
Alisema watuhumiwa hao walikutwa wakiiba transfoma ambapo polisi walipata taarifa za wizi huo kutoka kwa Wasamaria wema na kuweka mtego.
Aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Daniel Milanzi (32) na Shukuru Jemes (33) mkazi wa Buguruni wakiwa wanatumia gari namba SU 37150, aina ya Toyota Dyna, mali ya TANESCO waliyokuwa wakiitumia katika wizi huo.
"Gari linashikiliwa polisi kama kielelezo cha wizi huu, watuhumiwa wanaendelea kushikiliwa kwa mahojiano baada ya upelelezi kukamilika," alisema.
Kamishna Kova alisema, katika tukio lingine Agosti 13 mwaka huu, maeneo ya Mbezi Makabe, polisi waliokuwa doria walipata taarifa kutoka kwa Bw. Evaristi Masambinga aliyedai kuibiwa gari lake na majambazi wanne ambao waliondoka nalo.
Alisema baada ya polisi kupata taarifa hizo, walifanya msako mkali na kufanikiwa kulikamata saa nane usiku likiwa limetelekezwa umbali wa kilomita mbili kutoka eneo la tukio ambapo polisi wanaendelea kuwasaka majambazi hao.

No comments:

Post a Comment