20 August 2013

CAG AOMBWA KUKAGUA VYAMA VYA USHIRIKA


Na Grace Ndossa
WAZIRI wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Christopher Chiza amesema Mkaguzi wa Hesabu za Serikali (CAG), Ludovick Utouh anapaswa kukagua hesabu za vyama vya ushirika ili kubaini ubadhirifu uliopo. Kauli hiyo aliitoa Dar es Salaam jana wakati akiwasilisha Muswada wa Sheria Mpya ya mwaka 2013 kwa Vyama vya Ushirika mbele ya Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Kilimo, Mifugo na Maji
. Alisema kuwa, kamati hiyo inatakiwa kujadili na kutoa maoni yao na wadau juu ya muswada huo kabla ya kwenda kusomwa kwa mara ya pili bungeni. Alisema, vyama vya ushirika vimekuwa na changamoto nyingi kutokana na ubadhirifu wa fedha unaofanywa na viongozi hivyo wananchi kukosa imani na vyama hivyo.
Alisema, Muswada huo unaotarajiwa kusomwa kwa mara ya pili Agosti, 27, mwaka huu kwa ajili ya kubadilisha sheria hiyo iliyotungwa mwaka 2003 kwani haina makali ya kutosha kuwaadhibu viongozi. Naye Mwenyekiti wa kamati hiyo, Prof. Peter Msolwa alikiri vyama vya ushirika vimekuwa na migogoro mingi hali ambayo imepelekea wananchi kukosa imani na vyama hivyo. Alisema kuwa, muswada wa sheria hiyo mpya ya mwaka 2013 ikipitishwa na wabunge itakuwa ina nguvu ya kudhibiti ubadhirifu uliopo kwenye vyama hivyo.

No comments:

Post a Comment