26 August 2013

WASINDIKAJI ALIZETI WANG'AKA



Na Elizabeth Joseph, Dodoma
CHAMA cha Wasindikaji wa Mafuta ya Alizeti Tanzania (TASUPA) kimetoa siku kumi na nne kwa mmiliki wa Kiwanda cha Murzah Oil Mills Group of Companies kukanusha kauli yake aliyoitoa kudai kuwa mafuta ya alizeti hayana ubora kwa matumizi ya binadamu
. Rai hiyo ilitolewa juzi mjini hapa na Mwenyekiti wa chama hicho, Ringo Iringo wakati akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake na kuongeza kuwa mmiliki wa kiwanda hicho alitoa kauli ya kudai kuwa mafuta hayo hayajakidhi viwango na ubora kwa matumizi ya binadamu jambo ambalo halina ukweli ndani yake na kumtaka kuomba radhi kabla hatua kali za kisheria hazija chukuliwa dhidi yake.
Iringo alisema kuwa hata wateja wao kwa sasa wameingiwa na wasiwasi hali inayochangia kukosa soko la uhakika la mafuta hayo jambo linalosababisha kushuka kwa kipato kwa watengenezaji hao.
"Wasindikaji wa mafuta ya alizeti walipata hasara ya kiasi cha shilingi bilioni tano huku akitangaza kuwa alizeti ndiyo haina ubora jambo ambalo tunalipinga vikali kwani hata kiafya inashauriwa kuyatumia mafuta ya alizeti na tayari yalishathibitishwa na Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) na Shirika la Viwango (TBS)," alisema Iringo.
Hata hivyo alieleza kuwa chama hicho kipo tayari kwenda katika Tume ya ushindani kwa kushindanishwa ubora wa bidhaa hizo pamoja na kuandaa wanasheria wao ili kuhakikisha kauli hiyo inafutwa na kusafishwa ili kuondoa wasiwasi kwa watumiaji wa mafuta hayo.

No comments:

Post a Comment