28 August 2013

POLISI MBARONI KWA UJAMBAZI DAR

  • ALIKUWA NA WENZAKE WAPORA DOLA 20,000

 Na Masau Bwire

JESHI la Polisi Mkoa wa Ilala, linawashikilia watu wanne akiwemo askari wake mmoja kwa tuhuma za kufanya ujambazi kwa kutumia silaha (bastola) na kupora dola za Marekani 20,000, sawa na sh. milioni 32 za Tanzania.


Askari huyo amefahamika kwa jina la Mohamed Mhina ambaye kituo chake cha kazi ni Oysterbay, Mkoa wa Kipolisi Kinondoni, ambaye akiwa na wenzake wanne, walikwenda kufanya uhalifu nyumbani kwa mkazi mmoja wa eneo la Klabu ya Wazee,iliyopo Bungoni, Ilala, Dar es Salaam.

Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili, umebaini askari huyo alihamishiwa kituoni hapo akitokea Kituo cha Polisi Kimara,ambapo katika uhamisho wake alikuwa bado hajaanza kuutekeleza kwa sababu alikuwa likizo.Tukio hilo limetokea usiku wa kuamkia jana baada ya askari huyo na mwenzake, kupata taarifa kuwa kuna mtu ambaye si raia wa Tanzania aliyekuwa na fedha; hivyo walikwenda kumvamia nyumbani kwake ili wazichukue.

Watuhumiwa hao walifanikiwa kuingia nyumbani kwa mtu huyo, kumtaka awape fedha alizonazo na kupewa dola za Marekani 20,000 baada ya kumtisha kwa bastola.Wakati wakijiandaa kutoka nje ya nyumba hiyo, rafiki za mtu aliyevamiwa na kuporwa fedha hizo walifungua geti, kuingia ndani na kukuta hali tofauti; hivyo baada ya kuuliza kuna nini, aliyeporwa fedha hizo baada ya kusikia sauti za rafiki zake aliitika kwa sauti “nimevamiwa na majambazi”.

Wakati huo, askari huyo na wenzake walijificha nje ya nyumba hiyo na baada ya kusikia sauti hiyo, aliyekuwa na fedha hizo ambaye pia ndiye aliyekuwa ameshika bastola, aliruka ukuta na kutokomea kusikojulikana akiwaacha wenzake.Rafiki wa mtu aliyeporwa fedha hizo, walipambana na askari huyo pamoja na wenzake watatu ambao walichelewa kuruka ukuta na kufanikiwa kuwakamata.

Watuhumiwa hao wamefikishwa katika Kituo cha Polisi Msimbazi ambapo Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ilala, Marietha Minangi, alithibitisha kukamatwa kwa askari huyo na kusema taarifa zaidi juu ya tukio hilo atazitoa leo.Naye Kamanda wa Mkoa wa Kipolisi Kinondoni, Camilus Wambura, amekiri kuwa askari huyo alihamishiwa kituoni kwake, lakini amekamatwa kwa ujambazi.

Majina ya watuhumiwa wengine pamoja na nile la mtu aliyeporwa fedha hizo, hayakuweza kufahamika mara moja.Taarifa za uhakika kutoka kwa baadhi ya askari, zinasema mama mzazi wa askari huyo anafanya kazi ofisi moja na kigogo wa jeshi hilo Makao Makuu ya Polisi.  

1 comment:

  1. Polisi tena hao jamani!! Na utasikia kesi hii itaishia kimya-kimya na hakuna atakayechukuliwa hatua yeyote kwani mama mtu afanyakazi ofisini kwa kigogo!! Du! Dr. Emanuel Nchimbi upo? Nilifikiri uliyamaliza wiki iliyopita lakini naona kazi ndo tu wainza!

    ReplyDelete