28 August 2013

KURASINI WAFUNGA BARABARA KUSHINIKIZA KULIPWA HUNDI


Baadhi ya wakazi wa Mivinjeni Kurasini wakiwa na bango kando ya Barabara ya Kilwa, Dar es Salaam jana, lenye ujumbe wa malalamiko ya kudai kulipwa hundi za fidia ili kupisha mradi wa ujenzi wa bandari kavu kwenye eneo hilo.

 Na Waandishi Wetu

WAKAZI wa Mivinjeni Kata ya Kurasini wilayani Temeke jijini Dar es Salaam wanaotakiwa kuhama makazi yao ili kupisha mradi wa Mamlaka ya EPZ, wamefunga barabara ili kuishinikiza Serikali kuwalipa hundi zao na si viwanja.


Hali hiyo ilijitokeza jana wilayani humo, saa tano asubuhi ambapo wananchi walijipanga barabarani na kuzuia magari kupita, kwa madai wanaitaka Serikali iwalipe fidia zao ili waweze kuondoka katika eneo hilo.

Akizungumza na gazeti hili, Katibu anayefuatilia malipo ya wakazi hao, Judith George alisema kuwa wakazi hao wamelala barabarani kutokana na Serikali kuwapiga kuwazungusha pindi wanapotaka kulipwa hundi za nyumba zao ili waweze kuhama.

Alisema kuwa, viongozi wa Serikali pamoja na EPZ walifika katika eneo hilo Machi 13, mwaka huu na kufanya mkutano na wananchi kuhusu uwekezaji katika eneo hilo.

Alisema kuwa, mwekezaji alipozungumza nao walikubali kuhama ili kupisha ujenzi wa kiwanda katika eneo hilo la Mivinjeni na aliahidi kuwalipa fedha zao ili waweze kutafuta sehemu nyingine.

Aliongeza kuwa, mwekezaji huyo alifuatana na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Prof. Anna Tibaijuka na kuahidi wakazi hao kuwapatia viwanja mbadala katika eneo la Kigamboni karibu na Uvumba Kibanda.

Alisema kuwa, baada ya hapo Serikali ilishirikiana na Wilaya ya Temeke kufanya tathmini mwezi Aprili, mwaka huu ya nyumba zote za wakazi hao na kuweka alama za kubomoa.

“Baada ya tathmini Mkuu wa Wilaya ya Temeke, kwa kushirikiana na viongozi mbalimbali wa Serikali na mwekezaji walifanya tena tathmini na kubaini kuna nyumba 60 zina matatizo, eneo la Shimo la Udongo Kurasini,” alisema.

Aliongezea kuwa, baada ya kufanyiwa tathmini walitangaziwa kwamba Agosti 26, mwaka huu wafike wilayani kwa ajili ya kuchukua hundi zao, lakini walipofika waliambiwa mchakato wa utoaji hundi umesitishwa.

Hata hivyo, alisema kama mc h a k a t o wa u l i p a j i wa fidia umesitishwa kwa nini h awak u t a n g a z iwa k ama walivyofanya mikutano mara ya kwanza ya kuambiwa eneo hilo linahitajika na mwekezaji.

Naye mkazi mwingine wa eneo hilo, Mgeni Juma alisema Serikali imejaa porojo nyingi kutokana na mwekezaji kutoa fedha za kulipwa, lakini wao wanasitisha bila kutoa taarifa kwa wananchi.

Naye Rodi Panjo, mkazi wa Kurasini alisema, walipotangaziwa hundi zitaanza kutolewa Agosti 26, mwaka huu alisafiri kutoka Mbeya kuja kuchukua hundi yake, lakini alipofika alikuta mchakato huo umesitishwa.

“Na ukizingatia nalala nyumba za wageni, fedha ya kulipa nitapata wapi,” alihoji mkazi huyo.

Mkazi mwingine Gerad Mahinya alisema, biashara zao zimefungwa kutokana na nyumba hizo kuwekwa alama ya ‘X’ hali ambayo inawafanya wasijue hatima yao ya maisha.

“Wakazi wengi wameshahama kutoka maeneo hayo na wengine walikopa kutoka benki mbalimbali na kutafuta maeneo mengine ya kukaa, huku wakitegemea kupata fedha zao ili kulipa madeni,” alisema.

Naye Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kipolisi Temeke, Engelbert Kiondo aliwataka wakazi hao kuwa na subira na kufika Ofisi ya Mkuu wa Wilaya saa nane jana ili kupata majibu ni lini watapewa hundi zao.

Hata hivyo, aliwataka wakazi hao kuwa wavumilivu na kuachia magari yaweze kupita ili Alhamisi ya wiki hii, aweze kuwasiliana na Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, aweze kwenda kuzungumza nao katika ofisi ya Serikali ya mtaa wa Kurasini.

* Imeandikwa na Grace Ndossa, Theophil Ng’itu na Frank Monyo


No comments:

Post a Comment