04 July 2013

KINONDONI YAWATANGAZIA KIAMA MADEREVA WALEVI


 Na Anneth Kagenda
HALMASHAURI ya Manispaa ya Kinondoni jijini Dar es Salaam, imetangaza kuwa dereva yeyote mlevi akibainika amegonga taa mpya za sola zilizowekwa barabarani licha ya kulipa faini sh. 50,000 atalazimika kuzinunua mpya.
Taa hizo ni pamoja na zile ambazo zimewekwa jana katika Barabara ya Haile Selassie karibu na eneo la Masaki.
Hayo yalisemwa Dar es Salaam jana na Meya wa Manispaa hiyo, Yusuph Mwenda wakati wa hafla fupi ya kupokea mradi wa taa 107 zenye thamani ya sh. milioni 896 kutoka kwa Serikali ya China.

Alisema, waharibifu wengi wa taa hizo za barabarani ni madereva walevi; hivyo hatua hizo zikichukuliwa zitasaidia kupunguza kero hiyo.
“Lazima tufike mahali tukubaliane kuhusu mambo ya maendeleo, hizi ni taa zimewekwa kwa ajili ya kuwasaidia wananchi wetu, lakini utakuta dereva anaivamia na kuigonga...hatutakubaliana nao watazilipa taa zetu mara moja,”alisema Mwenda.
Alisema, manispaa hiyo ipo tayari kununua taa zingine kwa ajili ya kuzisambaza katika maeneo mbalimbali hususan mitaani, hivyo wataangalia uwezekano wa kuomba wapunguziwe bei.
Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Alphayo Kidata alisema Serikali inaipongeza China kwa kufikia maamuzi ya kuwasaidia wananchi kwa kuwawekea taa za sola.
“Jamani wananchi tunaomba mzitunze taa hizo, kwani zipo kwa ajili yenu, madereva chondechonde msizigonge kwani kufanya hivyo ni kuwakatisha tamaa wenzetu waliotupa msaada huu, lakini ikumbukwe kwamba zinatusaidia kwenye kumwulika,” alisema.
Balozi wa China nchini Tanzania, Lu Youging alisema, lengo la kufanya hivyo ni kutokana na ushirikiano uliopo baina ya nchi hizo mbili.


No comments:

Post a Comment