04 July 2013

KIKWETE AAGIZA EPZA IWAJENGEE WANANCHI


 Rachel Balama na Rehema Maigala
RAIS Jakaya Kikwete, ameiagiza Mamlaka ya Uwekezaji nchini (EPZA), kuhakikisha wananchi wanaohamishwa katika maeneo ya uwekezaji, kuwatafutia viwanja na kuwajengea nyumba ili kuepusha migogoro inayoweza kutokea kati ya wananchi na wawekezaji.
Alisema tatizo la wananchi kuvunjiwa maeneo yao na kulipwa fidia ya fedha inachangia mgogoro mkubwa kwa wananchi, hivyo mamlaka husika iwajengee nyumba na kuwawekea maeneo ambayo yatawasaidia kujiendeleza kiuchumi.
Rais Kikwete aliyasema hayo Dar es Salaam jana alipotembelea Banda la EPZA lililopo kwenye Viwanja vya Maonesho ya Biashara ya Kimataifa (Sabasaba).

Awali, Mkurugenzi wa EPZA, Dkt. Adelhelm Meru, alimhakikishia Rais Kikwete kuwa miradi ya ujenzi wa viwanda na bandari umeshasainiwa, bado utekelezaji wake.
"Kumekuwa na utaratibu wa wananchi kuvunjiwa nyumba zao na kulipwa fidia ya fedha; hivyo kushindwa kujikwamua kiuchumi, utaratibu huu siutaki uendelee kutumika ni vyema kila mwananchi ajengewe nyumba inayolingana na aliyovunjiwa.
"EAPZ haina budi kuhakikisha wananchi wanapohamishwa wanapewa viwanja, kujengewa nyumba na kuangalia kama maeneo wanayopelekwa yana fursa za kibiashara," alisema Rais Kikwete.
Aliwashukuru viongozi wa Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara nchini (TANTRADE); na kuwataka waimarishe ulinzi katika viwanja hivyo ili kuepusha madhara yanayoweza kujitokeza wakati wowote.
Alisema katika viwanja hayo, kunapaswa kufungwa kamera za uchunguzi ili kuepusha wi z i u n a o e n d e l e a amb a o unahatarisha usalama wa bidhaa za wafanyabiashara na wananchi wanaofika kupata mahitaji.
Pia Rais Kikwete alitembelea Banda la Mamlaka ya Ufundi Stadi (VETA); na kuitaka mamlaka hiyo ishirikiane na viwanda ili kuongeza ujuzi wa teknolojia za kisasa ambazo kwenye baadhi ya viwanda hakuna.
Aliongeza kuwa ni vyema teknolojia zinazotumiwa na VETA, zikasambazwa kwenye kampuni nyingine ili iweze kuharakisha maendeleo na kukuza uchumi.
Akizungumzia ujenzi wa nyumba za kibiashara na viwanda katika eneo la Kurasini, Dkt. Meru alisema kuwa mradi huo ni wa ubia kati ya Serikali ya China na Tanzania.
Alisema China itatoa fedha sh. bilioni 600 kwa ajili ya ujenzi wakati Tanzania itagharamia ardhi na sh. bilioni 90 kwa ajili ya ulipaji wa fidia na tayari sh. bilioni 25 zimetengwa kwa ajili ya fidia awamu ya kwanza.
Aliongeza kuwa, mradi huo ukikamilika utatoa ajira kwa watu 25,000 ambapo Watanzania hawatatumia fedha nyingi kwenda kununua bidhaa zao nje ya nchi bali bidhaa zote zitapatikana nchini.
Dkt. Meru alisema eneo la uwekezaji la Bagamoyo, mradi umetengewa sh. bilioni 50.2 na utaanza wakati wowote.
Naye Mkurugenzi Mkuu wa VETA, Zebadiah Moshi, alisema kwa sasa wamegundua mashine mpya zinazotumia kelele na miale ili kuzalisha umeme kwa matumizi ya nyumbani ambao hauna gharama kwa watumiaji.
Alisema kuwa sasa wanaendelea kuwafundisha wanafunzi teknolojia mpya ienee kila sehemu ili kuondokana na adha ya umeme..

No comments:

Post a Comment