20 February 2013

Kova: Tumeanza kuwasaka wahalifu



Mariam Mziwanda na Veronica Ikonga

JESHI la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, limeanza mikakati ya kudhibiti uhalifu na kuwakamata wahalifu katika
kipindi hiki ambacho wapo baadhi ya watu wanaotumia kivuli
cha dini na itikadi za kisiasa kutaka kuvuruga amani na utulivu uliopo nchini.


Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova, aliyasema hayo kwa waandishi wa habari na kusisitiza kuwa, jeshi hilo limejipanga kukomesha vitendo hivyo ambavyo vimeanza kuibuka kwa kasi katika jiji hilo.

“Uchumi wa nchi unategemea zaidi Jiji la Dar es Salaam kwa asilimia 80 na ndio Makao Makuu ya taasisi mbalimbali  na
Ofisi Kuu za Serikali hivyo usalama zaidi unahitajika.

“Jeshi la Polisi halipo tayari kuona uhuru wa itikadi za watu, unavurugwa na vikundi vya watu wachache na kuharibu amani
iliyopo, tutawakamata na kuwafikisha mahakamani,” alisema.

Alisema kwa hali ilivyo sasa, wananchi wengi wanaishi kwa hofu kubwa pamoja na kuogopa kufika maeneo ya katikati ya mji hasa kwenye baadhi ya siku zilizoanza kuchukua sura ya vurugu hivyo watu wote watakaokamatwa kwa kuvuruga amani, watashtakiwa kwa kosa la ugaini wa kuwajengea hofu wananchi.

Ametoa wito kwa wananchi kuendelea kutii sheria za nchi bila pamoja na kuwa wavumilivu wanapokuwa na madai mbalimbali kwani askari hawalipwi mshahara wa bure na Serikali bali kazi
kubwa iliyo mbele yao ni kuwadhibiti wote wanaokwenda
kinyume na sheria za nchi, kuchezea amani, usalama wa raia.

Akizungumzia sakata la Spika wa Bunge, Bi. Anne Makinda, kutumiwa ujumbe mfupi wa maneno (sms), wenye matusi katika simu yake ya mkononi, Kamanda Kova alisema jeshi hilo tayari linawashikilia baadhi ya watu waliotuma ujumbe wa matusi.

Alisema uchunguzi wa baadhi ya askari wanaodaiwa kuiba sh. milioni 150 zilizopolwa katika tukio la ujambazi Kariakoo,
aliwataka wananchi watambue kuwa, tayari mashtaka ya
askari hao kushtakiwa kijeshi yamekamilika.

“Tumeyafikisha kwa Mwanasheria wa Serikali, akibainisha aina
ya mashitaka wanayokabiliwa nayo, watafukuzwa kazi pamoja
na kuwafikisha katika vyombo vya sheria,” alisema.

No comments:

Post a Comment