18 February 2013

6 mbaroni vurugu za kuchinja Geita



Na Faida Muyomba, Geita

JESHI la Polisi mkoani Geita, limesema watu sita wamekamatwa wakituhumiwa kuhusika na mauaji ya Mchungaji wa Kanisa la
Pentekoste Assemblies of God (TAG), Mathayo Kachila, ambayo   yametokea hivi karibuni, Kijiji cha Buselesele, wilayani Chato.


Chanzo cha mauaji hayo ni vurugu zilizotokana na sakata la nani mwenye haki ya kuchinja kati wa Waislamu na Wakristo ambapo watu saba walijeruhiwa na kukimbizwa Hospitali ya Wilaya Geita, wawili kati yao walihamishiwa kwenye Hospitali ya Rufaa
Bugando, iliyopo jijini Mwanza.

Kamanda wa Polisi mkoani humo, Leonard Paulo, aliyasema hayo jana wakati akizungumza na waandishi wa habari.

Alisema watu wawili kati ya waliokamatwa, Khamis Abeid (44), mkazi wa kijiji hicho na Ramadhan Pastory (35), tayari wamefikishwa mahakamani.

“Mtu mwingine aliyefikishwa mahakamni hadi sasa ni Mchungaji wa Kanisa la Tanzania Assemblies of God (TAG), Isaya Rutha
Ikiri (52), kwa kosa la kuchinja wanyama bila kuzingatia sheria
ya chakula, dawa na sheria ya magonjwa ya mifugo,” alisema Kamanda

Aliongeza kuwa, jeshi hilo halipo tayari kuwataja watuhumiwa wengine ambao wanashikiliwa kwa tuhuma za mauaji hayo kutokana na sababu za kiusalama.

“Katika uchunguzi wetu juu ya mauaji haya, tutahakikisha tunatenda haki na Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP), imemtuma mwanasheria wake ambaye atashirikiana na jopo la askari wetu katika uchunguzi wa tukio hili,” alisema.

Aliwataka wananchi mkoani humo, kuwa watulivu ambapo jeshi
hilo litaendelea kuimarisha ulinzi katika maeneo mbalimbali.

No comments:

Post a Comment