21 August 2011

Wauza dawa kulevya wanyongwe-Wabunge

*Wapendekeza hivyo baada ya kuona mkanda wa video
*Mmoja alia akikumbuka watoto wa dadake waliokufa
*Pinda aahidi mahakama Maalum kwa wahalifu hao


Na Pendo Mtibuche, Dodoma

BAADHI ya wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania jana waliitaka
serikali kuchukua hatua za kuwanyonga wafanyabiashara wote wanaojihusisha na dawa za
kulevya. Walitoa kauli hiyo jana mjini hapa baada ya kuoneshwa mkanda wa wafanyabiashara hao hadharani.

Jana serikali iliwaonesha wabunge mkanda wa wafanyabiashara wa dawa za kulevya wakati wa kupitia semina iliyoandaliwa na Ofisi ya Waziri Mkuu na kuwafanya baadhi ya wabunge kuitaka serikali kuwachukulia hatua wahusika wote ya kunyongwa na badala ya kuwapa adhabu nyingine.

Mbunge wa Viti Maalumu Bi. Amina Mohamed Mwidau (CUF)  alimwaga machozi mbele ya wabunge wenzake na kushindwa kuendelea na mchango wake baada ya kueleza kuwa watoto wa dada yake walikufa kwa pamoja baada ya kuathirika na dawa za kulevya.

“Mimi nataka wafanyabiashara hawa wanyongwe mara moja,  wanaumiza watoto wetu, mimi watoto wa dada yangu walikufa wote kwa wiki moja kutokana na dawa hizo," alisema na  kushindwa kuendelea na ushuhuda huo kutokana na kububujikwa na machozi.

Baadhi ya wabunge waliopendekeza kunyongwa kwa wafanyabiashara hao ni pamoja na Mbunge wa Kasulu Mjini NCCR Mageuzi Bw. Moses Machali, Mbunge wa Mji Mkongwe Bw. Mohamed Sanya, Mbunge wa Mkanyageni (CUF) Bw. Mohamed Mnyaa.

Kwa upande wake Mbunge wa Kigoma Kusini NCCR Mageuzi Bw. David Kafulila naye alitaka wafanyabiashara hao wanyongwe ili walioajiriwa kwa unyongaji walipwe mishahara kihalali kwa kuwa kwa kipindi kirefu wamekuwa wakilipwa mishahara bila ya kufanya kazi.

Bw. Ferix Mkosamali wa Muhambwe (NCCR Mageuzi) aliwataka wabunge kuigomea bajeti ya Wizara ya Sheria isipitishwe hadi itoa majibu ya hakimu aliyetoa dhamana kwa wafanyabiashara wa madawa hayo ya kulevya.

Hata hivyo hali ilikuwa mbaya zaidi kwa Waziri wa Katiba na Sheria Bi. Celina Kombani ambaye alilazimika kusimama na kutolea ufafanuzi wa malalamiko ya baadhi ya wabunge
kuhoji kuhusu kuachiwa kwa raia wa Pakistani waliokamatwa na madawa nchini huku Watanzania waliokamatwa nao wakiendelea kusota ndani.

Waziri alieleza kuwa suala hilo limeshughulikiwa na tayari Mahakama ya Rufaa imekwishalisikiliza suala hilo lakini akasema kuwa zipo kasoro katika sheria huku baadhi ya wabunge wakipinga kwa sauti wakisema haiwezekani.

Kufuatia hali hiyo ilimlazimu Mwanasheria Mkuu wa serikali kuingilia kati suala hilo ambaye yeye kwa upande wake alisema kuwa biashara hiyo haramu ina fedha nyingi na inahitaji mtu wa kulifuatilia suala hilo kwa moyo thabiti wa kushinda vishawishi.

Alisema kuwa kuhusu suala la kesi ya Wapakistani kuachiwa huru tayari jambo hilo Jaji Mkuu alikwishaita jalada la kesi hiyo na kusema kuwa maamuzi ya kesi hiyo yatafanyika wiki ya kesho. Alisema kuwa mapungufu ya sheria ni kidogo lakini mapungufu ya binadamu ndiyo makubwa na kwamba baadhi ya wabunge wanapendekeza adhabu ya kifo, lakini si rahisi kuitekeleza.

"Mimi mwenyewe niliwahi kutoa adhabu ya kifo lakini nilipotoka nje ya chumba cha hukumu machozi yalinitoka hivyo hapa lazima tukubaliane kama tutaenda kwenye
adhabu hii," alisema.

Kikosi Kazi cha Kupambana na dawa za kulevya chini ya Kamishina Godfrey Nzowa kilikuja na orodha hiyo kwa wabunge huku sehemu kubwa ya waliokamatwa wakionekana kuwa ni raia wa kigen. Hata hivyo baadhi ya raia wa Tanzania walitajwa kwa sehemu kubwa kuwa nao ni sehemu ya mtandao huo ambao watoa mada walisema kuwa ni mawakala.

Hata hivyo kikosi kazi hicho kilisema kuwa si hao tu lakini wapo Watanzania ambao ni maajenti katika vita hiyo ambayo  kuwa ni ngumu na inahitaji msukumo wa aina yake
alisema mtoa mada ambaye kwa sababu za usalama jina lake linahifadhawa. 

Mtoa mada huyo alisema kuwa Kanisa Katoliki lilihususishwa kwa sehemu kubwa ambapo walisema kuwa katika Mkutano wa Papa Paul uliofanyika mwaka juzi, vijana wengi walitumia mwanya huo na kuzamia nje ya ambapo wengi walionekana kujihusisha na
madawa. Aliwataja baadhi ya waliokamatwa kuwa ni pamoja na Mchungaji Ikechuku Okidi wa Kanisa la lililopo Biafla jijini Dar es Salaam.

Wengine ni pamoja na Mzee wa Kanisa Raymond Gilbert Jungulu, Fred Chonde (Mkazi wa Mbezi) pamoja na mwanamtandao mkubwa wa dawa za kulevya Naima Mfundo  (Mama Lela)
ambao wamewezesha mapambano hayo kuwa ni makubwa.

Hata hivyo watoa mada hao walilalamikia kitendo cha mahakama kuwaachia kwa dhamana watuhumiwa wa dawa za kulevya ambao ni raia wa Pakstani wawili ambao walikamatwa kwa kilo 180 za Heroin. Alieleza kuwa kitendo hicho cha wao kufanya kazi kubwa ya kuwakamata wafanyabiashara hao kiliwavunja moyo pale  mahakama ilipowaachia kwa dhamana watuhumiwa wale.

Picha mbalimbali zilizooneshwa katika mkanda wa video hiyo, ziliwafanya wabunge kupandwa na jazba na kuanza kupiga kelele wakitaka watuhumiwa wanyongwe pamoja na Jaji na Mahakimu waliohusika kuwaachiwa huru raia hao. Bw. Nzowa alisema kuwa wamekuwa wakipata tabu kubwa licha ya mazingira ya kufanyia kazi kuwa ni magumu, lakini hawana hata chembe ya ulinzi.

Hata hivyo alisema kuwa wauza madawa hayo  hivi sasa  wameanza kujiingiza katika ufadhili w kisiasa ili kujaribu kujiweka katika mazingira mazuri jambo ambalo
alisema ni hatari kubwa.

Kwa upande wake Waziri Mkuu Mizengo akifunga semina hiyo  alisema kuwa serikali itajitahidi kufanya kila linalowezekana ili iweze kujenga mahakama maalumu kwa ajili
ya wauza dawa za kulevya. Aliwatahadharisha wapambanaji kuwa makini sana na mipaka ya nchi ambayo alisema inatumika zaidi katika kuvusha dawa kutokana na jiografia ya nchi.




4 comments:

  1. Haya ni mambo ya kusikitisha sana,unajua biashara hii ya madawa ya kulevya ni biashara yenye mitandao mikubwa sana,tuwe na kumbukumbu ya Mmexico aliyekuwa akiitwa Pablo Escoba,huyu bwana kwa biashara hii aliweza hata kuinunua serikali ili iweze kushamiri,alikuwa na uwezo wa kusema fulani auwawe na ikawa hivyo.Wamexico walikuja kupata nafuu ya hili pale rais wao wa miaka ya 90's alipokwenda kuomba msaada kwa Clinton rais ili Escoba auwawe,na ilikuwa ni vita kubwa sana.
    Tuone wenzetu China,waliliona hili miaka hiyo kuwa kizazi chao kama kitaingiliwa na ulevi wa aina hii basi itakuwa hatari kwa serikali na hata vizazi vijavyo,Kwanza waliondoa dhamana kwa wauza madawa ya kulevya,pia hakuna mahaka yao,mara utakapo
    kamatwa basi ni kunyongwa tuu,lakini binadamu ni kiumbe kilichoumbwa na tamaa,sheria iwe kali ya kunyongwa bila mahakama kama china kwani hii itasababisha mahakimu kuwa matajiri na biashara kushamiri kama jina la Tanzania lilivyo haribiwa mwaka uliokwisha nchi nyingi duniani,vijana wadogo wanabebeshwa hayo madawa na kukamatwa kwenye ma airport.
    Hili ni janga, Janga la kuharibu vijana,utawala wa jamii,haki kwa wanyonge na upotevu wa maadili,
    Tanzania haihitaji vyuo vya malezi ya wala madawa kwani mizizi inking'ka basi hatutakuwa na mbegu tena.

    Mungu wabariki wapambanaji
    Mungu wazidishie roho mbaya wauwaji

    Ameen

    ReplyDelete
  2. Mimi hapa sielewi kitu kimoja; ni vipi mharifu akamatwe kama mtu binafsi kwa makosa yake; harafu dini yake ihusishwe!!! Hapa kuna ubabaishaji mwingi. Mtenda maovu anapelekwa kwenye vyombo vya sheria bila kujali kama ni sheikh, mchungaji au muumini wa dini furani. Hapa hakuna uhusiano!!! Serikali isifanye siasa kwa kila jambo!!!

    ReplyDelete
  3. Kwa Mkristo msoma Biblia hawezi kushangaa,kwani biblia iko wazi ;kwamba "Wana wa Mungu walipokuwa wakienda kumwabudu Mungu wao,shetani naye alijihudhurisha nao".

    ReplyDelete
  4. Mimi sioni sababu gani kwa raia wa nje kuachiwa halafu wa ndani wanakula ugali keko.Hii biashara kuna watu wakubwa wanahusika ndio maana wanawafunga wasafirishaji wadogo na wa wakubwa wanapewa dhamana kwa kisingizio hitilafu ya viepengele vy sheri mbona kwa wabongo hakuna hitilafu hata kidogo?

    ReplyDelete