21 December 2010

Papic amtetea Mwape kuvurunda

Na Elizabeth Mayemba

KOCHA Mkuu wa Yanga, amewashangaa masabiki wanaombeza mshambulaji mpya wa timu hiyo, Mzambia Davies Mwape na kuwataka wasimtoe kasoro kwa mechi moja.Baadhi ya mashabiki wa soka wamekuwa na mtazamo tofauti kwa
mchezaji huyo, baada ya Yanga kufungwa na Azam mabao 3-1, huku Mwape ambaye aliingizwa dakika 20 za mwisho, kushindwa kuonesha uwezo mkubwa kwa mashabiki wake.

Akizungumza Dar es Salaam jana, Papic alisema haoni sababu ya watu kuanza kumponda mchezaji huyo, kwani kwa upande wake anaamini mchezaji huyo ni mzuri na atailetea mafanikio klabu hiyo.

"Mwape si mchezaji mbaya kama ambavyo baadhi ya mashabiki wanafikiria, tumpe muda na atafanya yale ambayo mashabiki walitarajia, lakini si vizuri kuanza kumtoa kasoro kwa mechi moja tu," alisema Papic.Alisema mashabiki wanatakiwa kuwa wavumilivu kwani anamfahamu vizuri Mwape, kuwa ni mchezaji mzuri ila kikubwa ni kumpa ushirikiano.

Mashabiki walioshuhudia mchezo kati ya Yanga na Azam, wengi wao hawakuridhishwa na kiwango cha Mwape, kutokana na kushindwa kutafuta mpira na pia alivurunda kwa kiasi kikubwa.

Kocha huyo alisema mechi ijayo ya kirafiki dhidi ya FC Leopards, atamuanzisha Mwape na anaamini atafanya vizuri pamoja na timu nzima.

No comments:

Post a Comment