21 December 2010

Uhuru Selemani apaa India

Na Elizabeth Mayemba

MCHEZAJI wa Simba, Uhuru Selemani ameondoka nchini jana kwenda nchini India kwa ajili ya kufanyiwa upasuaji wa goti aliloumia katika mechi ya mzunguko wa kwanza wa Ligi Kuu ya Bara na hivyo kushindwa kuitumikia timu yake kwa
mwezi mmoja.

Uhuru aliumia goti wakati timu yake ilipocheza na timu ya Toto African ya Mwanza, kwenye Uwanja wa CCM Kirumba.

Akizungumza Dar es Salaam jana kabla ya kwenda India, Makamu Mwenyekiti wa Simba Godfrey Nyange 'Kaburu', alisema wanakwenda India kwa ajili ya kumfanyia matibabu mchezaji wao Uhuru.

"Uhuru ni mchezaji mzuri katika timu yetu, hivyo kukaa kwake benchi kunatupa wakati mgumu ni matumaini yetu kwamba kila kitu kitakwenda vizuri tukifika India," alisema Kaburu.

Alisema wanataka kuimarisha timu yao kila idara, kabla ya kuanza kwa mzunguko wa pili wa ligi na mashindano ya kimataifa hivyo Uhuru, akipatiwa matibabu timu yake itakuwa kamili katika kila idara.Kaburu alisema hakuna mtu ambaye hafahamu uwezo wa Uhuru na anaimani kwamba hata mashabiki wa Simba, nao watafurahi kumuona tena Uhuru uwanjani.

Aliongeza kuwa gharama za matibabu ya mcheaji huyo itajulikana baada ya kufika India.

No comments:

Post a Comment