07 November 2010

Rais Museveni aonya wanaoeneza uongo.

KAMPALA,Uganda

RAIS wa Uganda,Bw. Yoweri Museveni amewaonya wapinzani kwa kueneza uogo kwa wapiga kura akisema kuwa wanaweza kuzuiwa kugombea ama
kufungwa jela.

Rais Museveni aliyasema hayo juzi wakati akihutubia mkutano wa hadhara katika viwanja vya shule ya msingi Angwecibange iliyopo katika Wilaya ya Dokolo ambapo aliwashauri wapiga kura kuandikisha maelezo yanayotolewa na wapinzani kwenye vituo vya polisi ili waweze kushughulikiwa.

“Wakazi wa  Lango mnapaswa kujikomboa wenyewe kuondokana na waongo.Kwa sasa wanazungumza kuhusu ardhi wakidai kuwa  NRM inataka kuiba ardhi,tupo serikalini kwa muda wa miaka 24 iliyopita wanaweza kutuonesha  ekari moja tuliyowahi kuiba,?”alihoji Rais Museveni.

“Kama hatujawahi kuiba ardhi katika kipindi cha miaka 42 iliyopita ni kwanini tuje kuiba ardhi katika eneo la Lango?”alihoji tena kiongozi huyo.


Rais Museveni,ambaye alipokea wanachama 54 kutoka chama cha  UPC alisema kuwa wale ambao wanadai kwamba Serikali ina mpango wa kupora ardhi wamekata tamaa na wanapaswa kuacha kuwachanyanya watu.



 “Kipindi kilichopita Kizza Besigye alikwenda katika eneo la  Amolatar na kusema kuwa Museveni ameuza ziwa Kyoga.Niliposikia jambo hilo niliripoti polisi na polisi walipomfuatilia akaamua kukimbilia mahakama ya katiba,”alisema.



Hata hivyo Dkt.Besigye mapema mwaka huu aliohojiwa na polisi baada ya kusema serikali imeuza ziwa  Kyoga kwa kampuni moja ya nchini Afrika Kusini.

Rais huyo aliongeza kuwa mtu yoyote anayeeneza uongo kama huo anapaswa kuzuiwa kugombea  na kawaagiza wapiga kura kuendelea kukiunga mkono chama cha National Resistance Movement (NRM) kwa sababu ndicho kina uwezo wa kushughulikia matatizo ya nchi.

 “Kabla ya mpango wa UPE,Wilaya ya  Dokolo ilikuwa na wanafunzi 24,000 lakini kwa sasa ina wanafunzi 50,000 idadi hiyo imeongezeka mara mbili,”alisema  kabla ya kuongeza kuwa huduma ya maji katika wilaya hiyo imeongezeka.

Alisema kuwa Serikali imetenga jumla ya sh bilioni 34 kwa ajili ya kuwalipa wanajeshi wa zamani na akasema kuwa pia wale ambao walipotea watafikiriwa.

No comments:

Post a Comment