Na Goodluck Hongo
Viongozi
wakuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) wametakiwa kutumia busara
katika maamuzi yao
juu ya tuhuma zinazomkabili aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho Bw.
Zitto Kabwe na wenzake ili kulinda masilahi ya chama ambacho msingi wake mkubwa
ni watu.
Mwenyekiti wa CHADEMA, Kanda ya Magharibi inayoundwa na
mikoa ya Kigoma, Katavi na Tabora, Bw. Mohamed Mambo, aliyasema hayo Dar es Salaam jana wakati
akizungumza na Majira kwa njia ya simu juu ya uamuzi wa Kamati Kuu,
uliomvua madaraka Bw. Kabwe na wenzake.
Wengine waliovuliwa madaraka ya uongozi ni Dkt. Kitila
Mkumbo aliyekuwa Mjumbe wa Kamati Kuu na Mwanazuoni wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam pamoja na
Bw. Samson Mwigamba, aliyekuwa Mwenyekiti wa CHADEMA, Mkoa wa Arusha ambaye kwa
sasa amesimamishwa uongozi.
Bw. Mambo alisema ni muhimu viongozi wakuu wa CHADEMA,
waangalie jamii inataka nini, kwa wakati gani ambapo Kamati Kuu ya chama hicho
ni kikundi cha watu wachache kinachotoa maamuzi ya wanachama wote hivyo maamuzi
hayo yaangaliwe vizuri.
“Umakini unahitajika katika jambo hili kwa masilahi ya chama
chetu...kamati kuu inaweza kutoa maamuzi yanayoweza kukigawa chama, wanachama
wapo tayari kufanya lolote juu ya maamuzi ambayo yatatolewa.
“Nimepokea simu nyingi kutoka mikoa mbalimbali ambayo wanapinga
Bw. Kabwe kuvuliwa nyadhifa zake za uongozi katika chama...maeneo mengi kadi za
CHADEMA zimerudishwa, wengine walikuwa wanasubiri maamuzi ya Zitto,” alisema
Bw. Mambo.
Aliongeza kuwa, kwa kuwa Bw. Kabwe amesema ataendelea kubaki ndani
ya chama, wanachama waliorudisha kadi nao wamesema wataendelea kubaki na kudai
wapo pamoja naye na wapo tayari kumfuata popote ambako atakwenda.
Bw. Kabwe na wenzake wanadaiwa kukihujumu chama hicho kwa kuandaa
waraka unaosema: ‘Mkakati wa Mabadiliko 2013’, hivyo Kamati Kuu iliwapa barua
za kujieleza ndani ya siku 14 kwanini wasifukuzwe uanachama kutokana na kosa hilo.
Hata hivyo, Bw. Kabwe juzi alizungumza na waandishi wa habari na
kudai kuwa, waraka uliotajwa si sababu ya yeye kuvuliwa nyadhifa za uongozi na
Kikao cha Kamati Kuu.
Alisema pamoja na kuvuliwa nyadhifa hizo, hatoki CHADEMA na
wanaotaka atoke, wamtoe wao na kwamba atakuwa wa mwisho kutoka na ana imani
kubwa na chama chake kuwa ndicho kinachostahili kuendesha nchi jana, leo na
kesho.
Aliongeza
kuwa, misukosuko inayoendelea ndani ya chama hicho ni mapambano ya kukuza
demokrasia si vinginevyo.
No comments:
Post a Comment