Na
Suleiman Abeid, Shinyanga
Wanachama wa vikundi
vya wajasiriamali wadogo katika kata ya Kitangili Manispaa ya Shinyanga wametakiwa kuepuka kuingiza siasa katika vikundi vinginevyo vitasambaratika
.
Tahadhari hiyo ilitolewa juzi na diwani wa viti maalumu (CCM)
manispaa ya Shinyanga, Mariamu Nyangaka, alipokuwa akizungumza na viongozi wa vikund imbalimbali vya wajasiriamali waliokutana kwa
ajili ya kuanzisha Chama cha Ushirika wa Akiba na Mikopo (SACCOS ).
Nyangaka alisema viongozi wa vikundi vya wajasiriamali pamoja
na wanachama wao kwa ujumla wanatakiwa kuhakikisha wanaendesha shughuli
zao bila kuingiza au kutanguliza itikadi ya vyama vya siasa katika vikundi vyao
kitu ambacho kinaweza kusababisha mgawanyiko miongoni mwao.
Alisema wapo baadhi ya wanasiasa wanaotumia wajasiriamali
wadogo kufikia malengo yao waliyojipangia huku wengine wakidiriki hata kuwazuia
wafuasi wa vyama vyao wasishirikiane na watu ambao si wafuasi wa vyama vyao vya
siasa hata kama shughuli zao zinapaswa kuendeshwa kwa ushirikiano wa pamoja.
"Ndugu zangu mkakati ambao mnataka kuuanzisha ni
mkakati mzuri utawasaidia kuendesha shughuli zenu kwa ufanisi mkubwa,
mtakapokuwa na SACCOS yenu itawasaidia kuweza kupata mitaji ya kuendesha
biashara zenu kupitia mikopo mtakayokopa yenye masharti nafuu tofauti na
inayotolewa na benki zetu nyingi nchini,"alisema.
"Lakini naomba mjihadhari na siasa katika vikundi
vyenu, mkimruhusu mdudu huyu kuwa miongoni mwenu eleweni wazi hamtadumu kwa
kipindi kirefu, hakikisheni mnaendesha shughuli zenu bila kuchanganya na itikadi
za kisiasa na wakemeeni wale wote watakaoonesha dalili za kuingiza siasa ndani
ya vikundi," alisema Nyangaka.
Kwa upande wake ofisa ushirika kutoka manispaa ya Shinyanga,
Athumani, alisema serikali kwa kipindi kirefu imekuwa ikihimiza umuhimu wa wananchi
kujiundia vyama vyao vya ushirika wa akiba na mikopo (SACCOS) kwa vile ni
rahisi zaidi kusaidiwa na asasi mbalimbali za kifedha. Alisema kupitia SACCOS
watu wengi wamefanikiwa katika biashara zao na baadhi wameweza kujenga nyumba
za makazi huku wengine wakisomesha watoto wao bila matatizo. Alisema jambo la
msingi ni uaminifu wa viongozi wa SACCOS zinazoanzishwa kwa kuhakikisha
zinakuwa na wanachama waadilifu na wenye kuzingatia sheria za uendeshaji wa
ushirika huo.
Katika hatua nyingine, viongozi hao wa vikundi vya wajasiriamali
wadogo wameunda uongozi wa muda utakaosimamia taratibu za uanzishwaji wa
ushirika wa akiba na mikopo.
Alisema utaundwa na vikundi vyote vilivyopo katika kata ya
Kitangili na kuhakikisha SACCOS hiyo inasajiliwa kisheria ili iweze kuanza kazi
mara moja.
Viongozi wa muda waliochaguliwa Elias
Joseph (Mwenyekiti), Richard Maige (mwenyekiti msaidizi), Patrick Kileo
(katibu), Masunga Elias (katibu msaidizi) ambapo Timothy Kakiri, alichaguliwa
kuwa mweka hazina.
No comments:
Post a Comment