13 November 2013

VIWANJA VIBOVU SABA VYASIMAMISHWA LIGI KUU



Na Fatuma Rashid
  Bodi  ya Ligi Kuu Tanzania (TPL Board), imefungia viwanja saba vilivyokuwa vikitumiwa na timu za Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) na Ligi Daraja la Kwanza (FDL), hadi vitakapofanyiwa marekebisho ili kukidhi mahitaji ya mechi za mpira wa miguu.

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana Ofisa Habari wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Boniface Wambura alisema uamuzi huo umefikiwa na TPL Board katika kikao chake cha kwanza kilichofanyika juzi ambapo pamoja na mambo mengine, kilipitia ripoti za mechi za VPL na FDL katika mzunguko wa kwanza.
  Alisema viwanja vilivyofungiwa na marekebisho yanayotakiwa kufanyika kwanza, ili viruhusiwe kutumika tena ni Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba (majukwaa yake yamechakaa, hivyo kuhatarisha usalama wa watazamaji) na Uwanja wa CCM Mkwakwani jijini Tanga (vyumba vya wachezaji kubadilishia nguo (dressing rooms) havina hadhi.
  Wambura alisema Uwanja wa Sokoine jijini Mbeya (sehemu ya kuchezea-pitch ni mbovu), Uwanja wa Sheikh Amri Abeid jijini Arusha (sehemu ya kuchezea ni mbovu), Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi (vyumba vya kubadilishia kutumika kwa ajili ya shule ya awali), Uwanja wa Majimaji mjini Songea (pitch ni mbovu) na Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro (pitch ni mbovu).
  Wambura ambaye ni Kaimu Katibu Mkuu wa TFF, alisema klabu ambazo timu zake zinatumia viwanja hivyo zimeshataarifiwa rasmi juu ya uamuzi huo, ambapo ama vinatakiwa kuwasiliana na wamiliki wa viwanja hivyo, ili wafanye marekebisho au kutafuta viwanja vingine vya kuchezea mechi zao.
  Wakati huo huo, timu za Taifa za Future Taifa Stars na Taifa Stars zinacheza leo. Mechi hiyo ya kirafiki itafanyika Uwanja wa Karume jijini Dar es Salaam kuanzia saa 10 kamili jioni.
  Mechi hiyo ni maalumu kwa Benchi la Ufundi la Taifa Stars linaloongozwa na Kim Poulsen, kuangalia wachezaji kumi kutoka Future Taifa Stars watakaoongezwa katika Taifa Stars, tayari kwa mechi ya kirafiki ya kimataifa itakayochezwa Novemba 19, mwaka huu jijini Arusha.
  Watazamaji 300 tu wataruhusiwa kushuhudia mechi hiyo kwa kiingilio cha sh. 5,000. Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager imeingia kambini jana. Miongoni mwa wachezaji wanaotarajia kuripoti ni kipa Ivo Mapunda wa Gor Mahia.

No comments:

Post a Comment