Neema Ndugulile
Timu ya Mbeya
City imepigwa faini ya sh. 500,000 na
Bodi ya Ligi Kuu Tanzania
(TPL Board) na kupewa onyo kali kwa timu yake ya U20 kutocheza mechi ya
utangulizi walipocheza na Yanga.
Akizungumza na waandishi
wa habari Dar es Salaam jana Ofisa Habari wa Shirikisho la Mpira wa Miguu
Tanzania (TFF) ambaye pia ni Kaimu Katibu Mkuu wa shirikisho hilo, Boniface
Wambura alisema pia Mbeya City wanatakiwa kulipa gharama za uharibifu, baada ya
mashabiki wao kuvunja kioo cha basi la Yanga, baada ya gharama hizo
kuthibitishwa na bodi hiyo.
"Pia Mbeya City
imepigwa faini ya sh. 500,000 kwa mashabiki wake kushambulia basi la wachezaji
wa Tanzania Prisons, baada ya mechi dhidi yao
na kulipa gharama za uharibifu baada ya kuthibitishwa na Bodi ya Ligi,"
alisema Wambura.
Alisema Coastal Union
imepigwa faini ya sh. 500,000 kutokana na vurugu za mashabiki wake ilipocheza
na Azam kwenye Uwanja wa Mkwakwani ambapo mwamuzi msaidizi, Hassan Zani
alishambuliwa kwa mawe na kujeruhiwa mkononi na kichwani, tukio lililosababisha
mchezo kusimama kwa dakika tatu.
Wambura alisema beki wa
Coastal Union, Hamad Khamis amepigwa faini ya
sh. 500,000 kwa kumpiga kichwa kwa makusudi Kipre Tchetche wa Azam. "Kitendo
hicho kilisababisha refa amtoe nje kwa kadi nyekundu, hivyo atakosa mechi tatu
zinazofuata za timu yake.
"Nayo Simba wamepigwa
faini ya sh. 500,000 kutokana na vurugu za mashabiki wake wakati wa mechi dhidi
ya Kagera Sugar," alisema Wambura.
Alisema adhabu zote
zimetolewa kwa mujibu wa kanuni. Pia Bodi ya Ligi imeahirisha kufanya uamuzi wa
mechi kati ya Stand United na Kanembwa JKT iliyochezwa Uwanja wa Kambarage, ili
kukusanya taarifa zaidi. Mechi hiyo haikumalizika. Bodi ya Ligi itakutana tena
Jumapili.
No comments:
Post a Comment