Na Fatuma Rashid
Kocha mpya wa timu ya Azam Fc anatarajiwa
kutua katika kikosi hicho mapema, kabla ya wachezaji wa timu hiyo kurudi
kambini.
Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana Msemaji wa timu hiyo,
Jaffer Iddi alisema wachezaji wote wamepewa likizo ya wiki mbili, hivyo uongozi
upo katika mchakato wa kutafuta kocha atakayerithi mikoba ya aliyekuwa kocha wa
timu hiyo, Mwingereza Stewart John Hall.
Msemaji huyo alisema kocha mpya atakapowasili, ndipo
atakapojua ni mchezaji gani atataka aanze naye na yupi amalize naye, kwani yeye
ndiye atakuwa akiufahamu uwezo wa wachezaji kuanzia mazoezini hadi katika
mechi.
Akizungumzia katika mechi ya mwisho ya mzunguko wa kwanza
ya michuano ya Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya Mbeya City,
Iddi alisema ilikuwa nzuri kuliko nyingine kwani wote walikuwa wazuri na
walipigana kutafuta nafasi nzuri katika kumalizia mzunguko huo.
Alisema timu yake kwa sasa
ipo mapumziko na itarudi kambini baada ya wiki mbili, ili kujipanga zaidi kwa
mzunguko wa pili wa ligi hiyo na michuano ya kimataifa.
Aliongeza kuwa, katika
mzunguko wa pili anaimani timu yake itakuwa vizuri zaidi kutokana na kuona
pamoja na kupima uwezo wa kila timu shiriki za Ligi Kuu, ambazo uwezo wake
wameshauona, hivyo anaona timu itajifunza kutokana na walichokiona katika
mzunguko wa kwanza.
Kocha Hall aliwaaga wachezaji na benchi la
ufundi, mara tu baada ya mchezo wa mwisho wa mzunguko wa kwanza dhidi ya Mbeya City
uliomalizika kwa sare ya mabao 3-3 kwenye Uwanja wa Azam Complex Chamazi, Dar es Salaam.
No comments:
Post a Comment