- ASHIRIKIANA NA MWANAYE KUMUUA MUMEWE
- KISA WIVU WA MAPENZI,POLISI WAZUNGUMZA
Na Esther Macha,
Mbeya
Mama na mtoto, wote wakazi wa Kijiji cha
Iseche, Kata ya Mwambani, Tarafa ya Kwimba, Wilaya ya Chunya, mkoani Mbeya,
wanatafutwa na Jeshi la Polisi mkoani humo kwa tuhuma za kumuua Silvester
Chikondo (55).
Akizungumza na gazeti hili jana, Kamanda wa Polisi mkoani
humo, Diwani Athuman, alisema marehemu alishambuliwa kwa marungu na mama huyo
ambaye ni mkewe na mtoto wake.
Alisema tukio hilo limetokea Novemba 12 mwaka huu, saa
mbili usiku katika Kijiji cha Iseche, wilayani humo.Aliongeza kuwa, marehemu
alikutwa na mauti wakati akitoka kilabuni kwenye pombe za kienyeji ndipo mama
huyo akiwa na mwanaye wa kiume, walianza kumshambulia.
Hata hivyo, Kamanda Athumani alisema marehemu
alipigwa marungu kichwani na kuongeza kuwa,
mama huyo anaitwa Husulina Kornel (42) na mwanaye Kondo Chikondo (19).
Akizungumzia mazingira ya
tukio hilo,
alisema marehemu alishambuliwa baada ya kufika nje ya nyumba yake ambapo chanzo
cha ugomvi huo ni wivu wa kimapenzi.
"Marehemu alionekana
akizungumza na mwanamke kilabuni ndipo mke wake alipoingiwa na wivu, ugomvi huo
ulianzia kilabuni, mke na mwanaye wamekimbia," alisema.
Alisema mwili wa marehemu
ulifanyiwa uchunguzi na kubainika ubongo kuchanganyika na damu hivyo
kusababisha kifo chake.
Hata hivyo, Kamanda Athumani ametoa wito kwa jamii hasa wanandoa,
kutatua matatizo yao
kwa njia ya mazungumzo si kujichukulia sheria mkononi kinyume cha sheria.
Alitoa wito kwa watu wenye taarifa za
watuhumiwa, wazitoe ili waweze kukamatwa na kufikishwa mahakamani. Pia
amewataka watuhumiwa hao, wajisalimishe wenyewe.
No comments:
Post a Comment