13 November 2013

MINARA KUPANUA SOKO LA MAWASILIANO NCHINI



 Na Mwandishi Wetu
  Imeelezwa kuwa kuanzishwa kwa kampuni huru za minara ya mawasiliano ya simu, kunaweza kupunguza gharama za uendeshaji kwa kampuni za simu za mkononi nchini, hivyo kuweza kusaidia kuleta ahueni kwa watumiaji wa simu hizo.

Kabla ya hapo kampuni zote za simu za mkononi nchini kila moja ililazimika kujenga mnara wake ambao unahitaji kiasi kikubwa cha uwekezaji ikiwa ni pamoja na matumizi ya jenereta, ulinzi na gharama nyingine za uendeshaji.
Hayo yalibainishwa jana na Mkurugenzi wa Mauzo na Masoko wa Kampuni ya Helios Towers, Michael Magambo wakati akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam.
"Hapo ndipo kampuni huru za minara zinapoingia. Humiliki, husimamia na huendesha minara, inayoweza kutumiwa na kampuni nyingi za simu kwa wakati mmoja na pia hata matangazo ya Tv, redio na mawakala wa hali ya hewa," alisema.
  Alisema, matumizi ya mnara mmoja huondoa mzigo wa gharama za uwekezaji wa miondominu pamoja na shughuli nyingine kwenye eneo la mnara.
  Pia alisema, kampuni za simu zinapata nafasi ya kuelekeza nguvu zaidi katika eneo wanaloliweza zaidi kutoa huduma za sauti na 'data' kwa Watanzania.
 "Wengi hawaufahamu mchango wetu katika kupanua huduma za simu Tanzania na Afrika kwa ujumla. Helios Towers ni kampuni kubwa ya minara huru nchini, ikiwa imejenga zaidi ya minara 1,000 ya Tigo Tanzania mwaka 2010, kisha ikajenga minara mingine 250 na inatarajia kuongeza mingine 150 ifikapo Desemba mwaka huu," alisema Magambo.
  Aidha, alisema kwa miaka miwili iliyopita, maeneo ya Helios yanayotumiwa kwa pamoja na kampuni za simu ni asilimia 53 kwa sasa na ni asilimia 60 ya maeneo mapya kwa nchi nzima huku ikisubiri uthibitisho wa serikali wa kuchukua minara ya Vodacom Tanzania.
"Tumekuwa tukisikia wakosoaji wakidai kwamba, kampuni kama Helios hayana ushindani kwa kuwa yamekamata soko kubwa.
  "Hii si kweli. Uhakika ni kwamba Helios imekuwa chachu ya kuwapo kwa ushindani kwenye soko la huduma za simu, ikiruhusu wageni kuingia kwenye soko na kuwapa nafasi watoa huduma kupeleka vijijini bila wasiwasi.
  "Mwishowe ni walaji ndio hufaidika zaidi kwa kupunguziwa bei za simu na kuchagua mtandao wanaoutaka. Ukweli ni kwamba tunafungua zaidi soko," aliongeza Magambo.
  Hata hivyo, katika kupunguza changamoto za kupeleka huduma maeneo ya vijijini yasiyo na huduma za simu, awali Serikali ilitoa gari lijulikanalo kama Universal Communication Action Fund (UCAF) linalosaidia kupunguza gharama na kuwahamasisha watoa huduma kwenda kwenye soko la vijijini.
  Hatua hiyo ilitokana na Sheria ya Upatikanaji wa Mawasiliano ya mwaka 2006 yenye lengo la kukuza maendeleo ya kijamii na uchumi mijini na vijijini kupitia TEKNOHAMA.Mbali na hayo Kampuni ya Helios iko mbioni kuweka mitambo 27 chini ya UCAF

No comments:

Post a Comment