Na Mwandishi Wetu
Kampuni ya Simu za Mkononi ya Airtel Tanzania
imeamua kupambana na changamoto zinazoikabili sekta ya elimu nchini kwa
kuzisaidia shule mbalimbali za sekondari kupata miundombinu ya kufundishia na
vifaa vya kujifunzia.
Pia kampuni hiyo kupitia
mradi wake wa Shule Yetu imewanufaisha wanafunzi wa Shule ya Sekondari Chalinze
iliyopo mkoani Pwani baada ya kukabidhi vitabu vya masomo ya sayansi vyenye
thamani ya sh. milioni tano kwa shule hiyo.
Akizungumza wakati wa
kukabidhi vitabu hivyo, Meneja Masoko wa Airtel Kanda ya Kusini na Mkoa wa
Morogoro, Aminata Keita alisema vitabu hivyo vitatumika katika kuongeza kiwango
cha uelewa na kukuza ufaulu kwa wanafunzi wa shule hiyo ambao walikuwa na
tatizo la uhaba wa vitabu.
"Vitabu
hivi...vitatumika kukuza ufaulu kwa wanafunzi maana wanafunzi wataweza
kujisomea kwa urahisi na kufuatilia masomo kwa ukaribu zaidi," alisema
Aminata.
Aliongeza kuwa, msaada huo
wa vitabu ni sehemu ya mpango mkakati wa kuzisaidia shule za kata
zinazolalamikiwa kufanya vibaya katika mitihani yao ya kitaifa.
"Tumetoa vitabu vya
masomo ya sayansi tukijua kabisa wanafunzi wengi hushindwa masomo hayo kwa
sababu mbalimbali, ikiwemo upungufu wa zana za kujifunzia ila nina imani mradi
huu wa Shule Yetu utaziwezesha shule za kata kufanya vizuri kwenye mitihani ya
kitaifa," alisema Aminata.
Kwa
upande wake mkuu wa shule hiyo, Emmanuel Kahabi alisema, upatikanaji wa vitabu
utarahisisha kazi ya ufundishaji kwa wanafunzi na pia wanafunzi wataweza
kuelewa kiurahisi maana zana za kufundishia zinapatikana
No comments:
Post a Comment