13 November 2013

MCHECHU ATUNUKIWA TUZO



 Na Grace Ndossa
   Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba (NHC), Nehemia Mchechu ametunukiwa tuzo ya uongozi bora pamoja na cheti kwa kutambua mchango wake mkubwa katika jamii na ndani ya shirika hilo.

  Tuzo hiyo ilikabidhiwa jana jijini Dar es Salaam na Rais wa Rotary Klabu ya Mzizima, Ambrose Nshala ambapo alieleza kuwa Mkurugenzi huyo amekuwa kiongozi bora na amethubutu kufanya kazi kwa ujasiri na kuonesha ndoto za kufika mbali.
  Alisema kuwa, Mkurugenzi huyo ni kijana mdogo, lakini ameonesha uthubutu wake katika kufanya kazi na mageuzi ndani ya shirika, hali ambayo imeonesha hatua kubwa kiuchumi na kazi anazofanya zitalifikisha mbali shirika.
  Alisema kuwa, Rotary klabu inathamini mchango wake na kutambua kazi aliyofanya kwa jamii kwani ni kubwa hivyo wametoa tuzo hiyo na cheti kwa ajili ya kuongeza hamasa kwa viongozi wengine kuiga mfano wa mkurugenzi huyo ili nchi iweze kupata maendeleo.
  Kwa upande wake, Mchechu alisema kuwa, tuzo hiyo itasaidia kuongeza hamasa zaidi katika kufanya kazi ili nchi iweze kupata maendeleo.
  Alisema kuwa, sera za Tanzania ni nzuri ila tatizo liko kwenye utekelezaji kwani viongozi wengi wanathamini maneno kuliko vitendo, hivyo ndiyo vinavyofanya mambo mengi kukwama.
  Pia alisema, sera nyingi hapa nchini nyingi huishia kwenye karatasi na nchi nyingi huiga sera za Tanzania katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ndiyo maana zimepiga hatua

1 comment:

  1. Mimi sidhani anastahiki tuzo yoyote. Kwanza shirika la NHC limejaaa rushwa, ubadhirifu na uzembe. Angalia jengo lililoporomoka na kuua watu 35 hapa jijini. Ingawa NHC ni mbia katika mradi huo yeye amesema hakuwa na habari kuwa jengo hilo liliongezwa magorofa kinyemela na kinyume cha sheria

    ReplyDelete