15 November 2013

MENO YA TEMBO Z'BAR, MSAKO MKALI



Na Mwajuma Juma, Zanzibar

  Jeshi la Polisi Zanzibar, linamtafuta ofisa mmoja wa Bandari ambaye anatuhumiwa kuhusika na usafirishaji meno ya tembo kupitia Bandari ya Malindi, visiwani humo.


Mbali ya kumsaka ofisa huyo, pia jeshi hilo limeanza kuwahoji baadhi ya watu na kufanya uchunguzi wa kina juu ya tukio hilo ili kuwabaini wahusika.

Akizungumza na waandishi wa habari jana, Kamishna wa Polisi Zanzibar, Mussa Ali Mussa, alisema watu wawili wanashikiliwa hadi sasa ambapo ofisa huyo wa Bandari bila kumtaja jina lake, anaendelea kutafutwa.

Alisema kazi ya kupakua mzigo na kuhesabu meno hayo tayari imekamilika ambapo kinachoendelea ni kufanya majumuisho ili kujua thamani halisi ya meno yaliyokamatwa.

"Vipande 1,021 vya meno ya tembo ndiyo vilivyokamatwa vikiwa katika magunia yenye uzito wa kilo 2,915, meno haya yalikuwa yasafirishwe kwenda nje ya nchi," alisema Kamishna Mussa.

Hata hivyo, alisema kuwa watu wawili wanaoshikiliwa wamekuwa wakirushiana mpira kila mmoja akimuhusisha mwenzake na mzigo lakini hadi jana, wahusika wa mzigo huo walikuwa hawajakamatwa.

"Watu wawili tunaowashikilia, mmoja anahusika na kampuni iliyokuwa isafirishe mzigo huu ya Island Sea Shells CO. LTD, tunaendelea kufanya uchunguzi ili kufahamu kama imesajiliwa Zanzibar au nje na wamiliki wake," alisema.
Aliongeza kuwa, kumetokea utata mkubwa juu ya nyaraka zilizokuwa zitumike kusafirisha mzigo huo ambao ulikuwa umehifadhiwa katika eneo la Darajabovu na baadaye kusafirishwa kwa gari hadi ndani ya Bandari ya Zanzibar.
 "Kuna mambo ya kutatanisha yamejitokeza kuhusu nyaraka za usafirishaji wa mzigo huu, tutaliweka wazi baada ya uchunguzi kukamilika,", alisema Kamishna Mussa.
  Alisema wingi wa mzigo huo, haujawahi kutokea Afrika Mashariki ambapo hilo ni tukio la tatu kutokea Zanzibar. Awali ilikamatwa kontena la meno ya tembo katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Zanzibar na tukio la pili lilitokea mwaka 2012 katika bandari ya Malindi Zanzibar.

 

No comments:

Post a Comment