15 November 2013

MAGUFULI AWAPIGA KIJEMBE UPINZANI



 Na Wilhelm Mulinda, Mwanza
  Waziri wa Ujenzi, Dkt. John Magufuli, jana aliweka jiwe la msingi kwenye daraja la waenda kwa miguu, katika eneo la Mabatini jijini Mwanza na kutupa kijembe kwa vyama vya upinzani vinavyodai daraja hilo linajengwa kwa gharama yao.

Akihutubia wananchi waliohudhuria tukio hilo, Dkt. Magufuli alihoji kuwa, kama daraja hilo linajengwa kwa gharama yao mbona hawakuweka jiwe la msingi wala kuhudhuria katika shughuli hiyo, hali iliyofanya wananchi kumshangilia.
Aliwaomba wananchi kumpuuza mtu yeyote ambaye atadai daraja hilo ni lake bali linajengwa na Serikali ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwa kutumia pesa za wazalendo.
Alisema ujenzi wa daraja hilo ni miongoni mwa ahadi za zilizotolewa na CCM kwenye ilani yake ya uchaguzi 2010 kwa lengo la kuboresha miundombinu ya barabara nchini.
"Maendeleo hayana chama, Serikali iliyopo madarakani inatekeleza miradi ya maendeleo kwa ajili ya watu wote bila kujali rangi wala itikadi za vyama zao, vyama vya siasa vinakuja na kupita lakini nchi iko palepale," alisema.
Awali akisoma taarifa ya mradi wa daraja hilo, Meneja wa Wakala wa Barabara nchini (TANROADS), mkoani humo, Mhandisi Leonard Kadashi, alisema ujenzi wa daraja hilo unafanywa na Kampuni ya Ujenzi ya Nordic kutoka Dar es Salaam.
 Aliongeza kuwa, TANROADS mkoani humo, walishauri ujenzi huo baada ya watu wengi kupoteza maisha kwa kugongwa na magari wakati wa kuvuka barabara eneo hilo ambalo lina watu wengi.
Alisema mwaka huu, watu 12 wameshapoteza maisha kwa kugongwa na magari na wengine kupata ulemavu kutokana na ajali za mara kwa mara.
  Katika hatua nyingine, Dkt. Magufuli alisema Serikali ina mpango wa kutengeneza njia nne kwenye Barabara ya Mwanza- Uwanja wa ndege jijini humo ili kukabiliana na msongamano wa magari.

No comments:

Post a Comment