13 November 2013

MAZITO YAMKUTA MBUNGE LEMA



  •  ACHAFULIWA MTANDAONI, AITUHUMU UVCCM TAIFA
Queen Lema, Arusha na Mariam Mziwanda, Dar
  Katika hali isiyo ya kawaida, Mbunge wa Arusha Mjini, Bw. Godbless Lema, ameutuhumu uongozi wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM), Taifa kwa mada ya kusambaza picha zinazoonesha akiingiliwa kinyume na maumbile katika mitandao ya kijamii.

  Mbali ya uongozi huo, Bw. Lema pia alimtuhumu Mwenyekiti wa UVCCM Taifa, Bw. Sadifa Juma Khamis, kwa kushiriki kumchafua hivyo amemtaka Spika wa Bunge, Bi. Anne Makinda, achukue hatua na kudai ushahidi wa jambo hilo upo hadharani.
  Bw. Lema aliyasema hayo Mjini Arusha jana alipokutana na waandishi wa habari ili kuzungumzia jambo hilo na kusisitiza kuwa, suala hilo limemsikitisha sana. “Ushahidi wa namba za simu zilizohusika kusambaza picha hizo upo, Khamis (Mwakilishi Jimbo la Donge, Zanzibar), anahusika na udhalilishaji uliofanywa na vijana wa UVCCM Taifa,” alisema Bw. Lema.
  Alisema picha hizo zimesambazwa katika mitandao ya kijamii na watumiaji wa simu za mkononi zikiwa na ujumbe unaodai Lema akilawitiwa na wanaume wenzake.Aliongeza kuwa, Oktoba 29 mwaka huu, mkewe aliyemtaja kwa jina la Bi. Neema Lema, alipata picha hizo zilizotumwa moja kwa moja katika simu yake zikiwa na ujumbe usemao “Hiyo ndiyo kazi anayoifanya mume wako”.
   Bw. Lema alisema, suala hilo halikuishia hapo kwani picha hizo zilitumwa kwa mama mkwe wake na kusababisha familia ya mke wake na wazazi wake kukosa amani “Mke wangu alitumiwa picha hizi katika mtandao wa WhatsApp na baadaye ilisambazwa zaidi hadi kwa wapigakura wangu jimboni na kudai ndiyo kazi inayofanywa na Mbunge wao,” alisema.
  Aliongeza kuwa, uchafu huo ulikuwa ukifanyika wakati akiwa bungeni Dodoma ambapo Bw. Khamis, alionekana akisambaza picha hizo kutoka kwenye kompyuta yake (mpakato), kuwapa wabunge jambo ambalo lilichangia amani ya bunge kuharibika siku hiyo.
 “Wakati picha hizi zikisambazwa, nilijulishwa suala hili na wabunge wanawake wa CCM, ilibidi niende kwa Spika ambaye alikiri picha hizo zimesababisha akose morali ya kuendesha vikao. “Pia nilizungumza na uongozi wa Bunge nikilalamikia kudhalilishwa kwa kutengenezewa picha zinazoonesha nikiingiliwa na wanaume wenzangu... Spika aliahidi kulishughulikia,” alisema Bw. Lema.
  Bw. Lema alisema, kutokana na picha hizo, bado hazimnyimi kinga ya kuendelea kusema ukweli juu ya jambo lolote badala yake ataendelea kupambana ili kuwatetea wanyonge.“Kamwe siwezi kuwatafuta waliotengeneza picha hizi na kuzisambaza kwenye mitandao na simu za watu bali atawasaidia viongozi wa UVCCM kuzisambaza kwenye Makanisa, Misikiti, mikutano ya hadhara ili kuwaonesha wananchi ukatili dhidi yake unavyozidi kushika kasi asiwe na sauti ndani ya nchi,” alisema.
  Wakati huo huo, Mke wa Mbunge huyo, Bi. Neema, alisema hicho ni kitu kidogo sana dhidi ya mumewe na waliofanya vitendo hivyo walilenga kuvunja ndo yake lakini haitatokea. Sadifa azungumza
  Akijibu tuhuma hizo akiwa njiani kwenda nchini Ethiopia, Bw. Khamis alisema jumuiya hiyo au yeye mwenyewe hawezi kutumia cheo chake kufanya vitendo hivyo.
  “Mimi na Mheshimiwa Lema wote ni wabunge, tofauti yetu ipo katika vyama na majimbo...tomefahamiana bungeni na wala simjui kwa undani, tuhuma dhidi yangu si za kweli kwani siwezi kufanya kitendo hicho ambacho si cha kibinadamu hata kama tuna tofauti za kisiasa.
 “Mimi ni Muislamu na dini yangu hairuhusu kufanya hivyo, binafsi sijui kutumia kompyuta na Mheshimiwa Lema analijua hilo...hivi sasa Ofisi ya Bunge imeanza kutoa mafunzo kwa wabunge wasiojua kutumia kompyuta, nami najifunza,” alisema.
  Alisema simu anazomiliki ni mbili, moja ni Nokia ya tochi na nyingine ya kichina yenye laini tatu na hajui kama simu hizo zina mitandao na hajawahi kujaribu.Bw. Khamis aliongeza kuwa, hulka yake hayupo karibu na makundi yanayoweza kumuingiza au kumshawishi afanye vitendo hivyo hivyo yupo tayari kukutana na Bw. Lema kwa amani ili wazungumze na kuwasaka waliofanya vitendo hivyo ambavyo si vya kistaarabu.
“Mheshimiwa Lema akinitafuta nitampa ushirikiano, ninachokijua mimi, mwenzangu ananitafutia umaarufu kwa sababu pamoja na vyeo nilivyonavyo bado sifahamiki sana.
  “Natumia cheo changu ndani ya UVCCM kuijenga jumuiya na CCM... kwanza namuomba radhi kwa sababu tayari ana imani potofu dhidi yangu, pili namshauri afanye utafiti,” alisema.
Alisema imani yake ni kwamba, tofauti zao kisiasa haziwezi kumshawishi afanye vitendo hivyo kwani ipo siku Bw. Lema anaweza kurudi CCM na kufanya naye kazi pamoja.
  Aliongeza kuwa, umefika wakati wa Bw. Lema kukumbuka kuwa, tofauti za kisiasa zilizopo ndani ya chama chao pia zinaweza kutumika kumchafua katika mitandao





5 comments:

  1. Yeye mwenyewe athibitishe kama ni uongo au la

    ReplyDelete
    Replies
    1. Muoshwa huoshwa maumivu anayoyapata kwakusingiziwa ndivyo na wengine anaowatuhumu na kuwasingizia wanayapata busara itumike

      Delete
  2. WAKATI WENGINE WANAUMIZA VICHWA KUANGALIA MAENDELEO YA TAIFA YAKUWAJE,WAO NA MAJUNGU YA MTANDAONI.LEMA SONGA MBELE USIFE MOYO WAENDELEE KUPOTEZA MUDA WAO.SONGA MBELE KAMANDA.

    ReplyDelete
  3. MAELEZO HAYA YA BWANA KHAMIS YANAPINGANA NA TAARIFA YA UVCCM. MAALEZO HAYA ANGALAU YANA UUNGWANA NDANI YAKE LAKINI YALE YA UVCCM NI UUPUUZI MTUPU. KAMA HALI NDIYO YA KUCHAFUANA KIASI HICHO WA KULAUMIWA NI WANANCHI. TUMESHINDWA KUCHAGUA VIONGOZI

    ReplyDelete
  4. Tanzania tunasema kuna amani, iko wapi hiyo amani kama m2 akitaka kukuchafua anakuchafua 2 awezavyo? siasa zinaliacha taifa la Tanzania kuwa MASIKINI.

    ReplyDelete