28 November 2013

LHRC YATAKA KATIBA MPYA IOKOE MUUNGANO



Na Mariam Mziwanda
  Muungano wa Tanzania na Zanzibar umefananishwa na mgonjwa aliyelazwa kwenye Chumba cha Wagonjwa Mahututi (ICU), hivyo Watanzania wametakiwa kuunusuru kupitia Katiba Mpya inayotarajiwa kupatikana kabla ya uchaguzi mkuu ujao mwaka 2015.

Kauli hiyo ilitolewa jana jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi wa Utetezi na Maboresho wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Harold Sungusia, wakati akifungua mkutano wa siku tatu wa asasi za kiraia.
Alisema ni muhimu kwa wananchi kupewa fursa ya kujadili Muungano na kuufahamu kwa kina kuwa unahitajika ili kuepukana na chuki zinazopandikizwa kutoka kwa wanasiasa wenye uchu wa madaraka.
“Kuna wanasiasa wachache wanaotumia nafasi zao ndani ya jamii kupotosha wananchi kuhusu muungano, wanapandikiza chuki kwa ahadi za kisiasa ili wapate madaraka,” alisema.
Aliongeza kuwa elimu ya faida za Muungano ikiwafikia vizuri wananchi na kupewa fursa ya kujadili ipasavyo kwa muda uliopo kabla ya Bunge la katiba inatosha kuufanya hudumu na kuwa matunda kwa vizazi vijavyo.
Alisema Muungano uliopo unategemea kufa au kupona kutokana na maamuzi ya nchi kupitia katiba mpya kwani umegubikwa na kero nyingi ambazo kwa muda mrefu hazijapatiwa tiba.
“Muundo wa Muungano ni tatizo hususani katika uundaji wa Serikali yenyewe hali inayosababisha wananchi wa pande zote mbili kulalamika, lakini wakati uliopo unatosha kupitia Bunge la katiba kunusuru muungano ulipo,” alisema.
Akileleza changamoto kubwa ambazo wananchi wanatakiwa kuzipatia majibu kupitia katiba mpya ili kuwa nyenzo ya uhai wa Muungano huo alisema ni pamoja na utatuzi wa suala la mapato katika mgawo wa asilimia nne kwa Zanzibar na uwepo wa uhuru wa kuchagua viongozi.
Kwa upande wa mjumbe wa AZAKI takriban 36, Baraka Mohamed Shamte, alisema Watanzania bado wanahitaji Muungano na kwamba jambo la muhimu ni kujadili matatizo yaliyopo na kuyafanyia kazi ili uendelee kudumu.
“Kuanzishwa kwa Muungano hakukuwa kwa bahati mbaya historia ya Muungano wananchi wake ni wamoja, vijana wa leo wakishasoma na kupata shahada wanafikiri wanafahamu kila kitu, kulikuwa na sababu tosha za kuungana kwa nini Muungano huo haukuwa na Kenya nchi nyingine ni vyema kuwa wa kweli katika kuzungumzia Muungano,” alisema.
Kwa upande wake Ramadhan Suleiman Nzori aliwataka vijana wasomi kutambua kuwa wanategemewa sana katika kulinda na kuthamini Muungano na wasichukue vitu vidogo vidogo na kuona ni rahisi kuvunja Muungano uliopo.

No comments:

Post a Comment