06 November 2013

KIVUMBI CHA LIGI KUU KUTIMKA LEO



Na Fatuma Rashid
  Pazia la michuano ya Ligi Kuu Tanzania Bara (VPL), mzunguko wa kwanza linafungwa leo kwa mechi tano kupigwa viwanja tofauti nchini.

  Katika mechi hizo Simba yenye pointi 21 inayoshikilia nafasi ya nne katika msimamo wa ligi hiyo itakuwa wenyeji wa Ashanti United katika mechi itakayochezwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
 Simba itaingia uwanjani ikisaka pointi tatu kwa udi na uvumba, baada ya kushindwa kufanya hivyo katika mechi nne zilizopita ambapo ilitoka sare tatu na kufungwa moja.
 Ashanti United imefikisha pointi 10 na kushika nafasi ya 11 katika msimamo wa ligi hiyo yenye timu 14.JKT Ruvu inayoshikilia nafasi ya 9 naye itashuka katika Uwanja wa Chamazi Complex
kuumana na ‘Wagosi wa Kaya’ Coastal Union inayoshika nafasi ya 7 kwa kuwa na pointi 16.
  Nayo Kagera Sugar itaikaribisha Mgambo Shooting katika Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba..Kwa upande wake Rhino Rangers yenye pointi 11 iliyopo nafasi ya 10 watawakaribisha Tanzania Prisons yenye pointi 8 ikiwa nafasi ya 12 katika Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi mjini Tabora.
  Nayo Ruvu Shooting wakiwa na pointi 14 iliyopo nafasi ya nane, watajitupa katika Uwanja wa Uwanja wa Mabatini kuikaribisha
Mtibwa Sugar ambayo ina pointi 19 wakiwa nafasi ya tano.Timu zote zinapigana kuhakikisha zinapata pointi tatu muhimu, ili kujiweka vyema katika msimamo wa ligi hiyo

No comments:

Post a Comment