Rais Dkt.Jakaya Kikwete na mkewe Mama Salma Kikwete wakifariji familia ya Marehemu Dkt. Sengodo Mvungi nyumbani kwao Kibamba Dar es Salaam jana.
- SALAMU ZA RAMBIRAMBI ZAZIDI KUMIMINIKA
- MWILI WAKE KUWASILI KESHO,KUAGWA JUMAMOSI
Na Waandishi Wetu
Rais Jakaya Kikwete, amesema ameshtushwa na
kufadhaishwa na taarifa za kifo cha Mjumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba,
Dkt. Sengondo Mvungi, kilichotokea juzi kwenye Hospitali ya Milpark, Johannesburg, Afrika
Kusini.
Katika salamu za rambirambi ambazo amemtumia Mwenyekiti wa
Tume hiyo, Jaji Joseph Warioba, Rais Kikwete alisema amepokea kwa mshtuko
mkubwa na taarifa za kifo cha Dkt. Mvungi.
"Kwa hakika ni taarifa iliyonisumbua na kunipa huzuni
kubwa," alisema Dkt. Kikwete. Rais Kikwete alisema hakuna shaka kuwa
katika maisha yake Dkt. Mvungi alitoa mchango mkubwa katika maendeleo ya Tanzania kwa namna mbalimbali na kuwa kifo
kimemfika wakati Taifa la Tanzania
lilikuwa bado linahitaji busara, hekima na mchango wake katika mchakato mzima
wa kusaka Katiba mpya.
"Kuanzia alipokuwa mwandishi wa
habari katika Magazeti ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya Uhuru na Mzalendo, hadi
uhadhiri wake katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, hadi uwakili katika Kampuni
ya South Law Chambers, hadi uongozi wake katika Chama cha NCCR-Mageuzi, hadi
uamuzi wake wa kugombea Urais wa Tanzania mwaka 2005 na sasa akiwa Mjumbe wa
Tume ya Katiba, Dkt. Mvungi ametoa mchango wake mkubwa sana katika maendeleo ya nchi yetu. Na hili
sitalisahau," alisema Rais Kikwete na kuongeza;
"Kwa masikitiko makubwa, nakutumia wewe Jaji Joseph
Warioba, Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba salamu za rambirambi za
dhati ya moyo wangu nikiomboleza kifo cha Dkt. Mvungi.
“Nakupa pole nyingi wewe Mwenyekiti, wajumbe wa Tume na
wafanyakazi wote wa Tume kwa kuondokewa na mwenzenu. Naungana nanyi kuombleza
msiba huo mkubwa.
“Kupitia kwako, natuma pole nyingi kwa wana-familia, ndugu,
marafiki na majirani wa Dkt. Mvungi kwa kuondokewa na mhimili, msimamizi wa
familia na ndugu.
“Wajulishe kuwa niko nao katika msiba huu mkubwa. Wajulishe
kuwa msiba wao ni msiba wangu pia. Muhimu waelewe kuwa binafsi naelewa machungu
yao katika
kipindi hiki kigumu na namwomba Mwenyezi Mungu awape subira waweze kuvuka
kipindi hiki kigumu kwa sababu yote ni mapenzi yake.
Mbatia anena
Wakati huo huo, mwili wa Dkt. Mvungi unatarajia kuwasili
nchini kesho na utapokelewa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu
Julius Nyerere na kisha kupelekwa nyumbani kwake Kibamba Msakuzi.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam
jana, Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia, alisema baada ya mwili huo
kuwasili itafanyika misa takatifu katika Kanisa la Mt. Joseph
saa nne asubuhi Jumamosi.
Alisema baada ya misa hiyo saa sita mchana mwili wake utapelekwa
viwanja vya Karimjee kwa ajili ya kuagwa na kisha kusafirisha kwenda Mwanga,
mkoani Kilimanjaro kwa ajili ya maziko.
Alisema katika kipindi hiki cha msiba bendera za chama
hicho zitapepea nusu mlingoti kwa muda wa wiki moja.
Waziri
Chikawe
Naye Waziri wa Katiba na Sheria, Mathias Chikawe, alisema
msiba huo ni pigo kwa taifa kwani marehemu alikuwa ni kiungo muhimu na alitumia
ujuzi, elimu na nafasi aliyonayo kwa jamii hasa katika kipindi hiki muhimu cha
mchakato wa katiba mpya.
Alisema ni wananchi waelewe kuwa ikitokea kuyumba au kuwepo
kwa pengo lolote katika mchakato huo basi litakuwa limechangiwa na kutokuwepo
kwake Dkt. Mvungi.
Jaji
Warioba amlilia
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba
Jaji Joseph Warioba, alisema Dkt. Mvungi ni mtu muhimu ambaye alikuwa na
mchango mkubwa kwenye Tume yake.
Alisema alitumia utaalam wake wa sheria na uzoefu katika
kuhakikisha hoja zake alizokuwa akizitoa anazisimamia ipasavyo.
CUF
yatuma rambirambi
Kwa
upande wake Chama cha Wananchi (CUF), kimesema kimepokea kwa mshituko na
majonzi makubwa taarifa ya kifo
cha Dkt. Mvungi.
"Kifo cha Dkt.Mvungi kimeishtua Tanzania nzima hasa kwa vile
tulitazamia kuwa angeishi kwa muda mrefu zaidi.
Kifo hicho kinazidi kusikitisha kwa vile kimetokana na
kushambuliwa kikatili na watu wasiojulikana wanaodaiwa kuwa ni majambazi,"
ilieleza taarifa ya CUF.
Mwenyekiti wa Taifa wa Chama cha Wananchi CUF, mimi mwenyewe na
viongozi waandamizi wa CUF walimjua vizuri sana Marehemu Dkt. Mvungi kwani
tulifanya kazi naye kwa karibu," alieleza taarifa ya CUF iliyotolewa na
Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad.
Maalim Seif, alisema Dkt. Mvungi alikuwa mpambanaji jasiri
asiyeyumba katika mapambano ya kuiletea Tanzania mfumo wa kidemokrasia
halisi unaolenga kulinda haki za kila Mtanzania bila ya ubaguzi wa aina yoyote
ile.
Alisema Dkt. Mvungi alichukia uonevu, manyanyaso, ukandamizaji na
dhuluma dhidi ya binadamu yoyote.
"Tulishirikiana naye kwa karibu katika mchakato wa kudai
Katiba mpya ya Tanzania
na pale vyama vya siasa vilipounda kamati ya kufanya rasimu ya Katiba mpya
Marehemu Dkt. Mvungi ndiye aliyekuwa Mwanasheria wa Kamati hiyo.
Alitoa mchango mkubwa katika kuandaa na kukamilisha rasimu
hiyo," alisema Maalim Seif na kuongeza;
"Wengi tulifarijika pale alipoteuliwa kuwa miongoni mwa
Wajumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba ya Tanzania.
Tulijua uwezo wake, umahiri wake, utendaji kazi makini wake na
dhamira yake ya kuona Tanzania
inapata Katiba nzuri kwa masilahi ya wananchi wote bila kujali itikadi za
vyama."
Alisema Dkt. Mvungi alikuwa ni wakili mahiri, msomi makini na
kiongozi shupavu.
Alisema alikuwa jasiri hasa katika kuwatetea wanyonge na katika
kutoa mawazo yake. Alikuwa ni mchambuzi hodari wa mambo ya kisheria, hasa
sheria inayoambatana na masuala ya Katiba.
Hali kadhalika alikuwa mchambuzi aliyebobea katika masuala ya
kijamii na ya kisiasa na aliguswa sana na
umuhimu wa kuendeleza elimu bora nchini Tanzania.
Maalim Seif alisema kifo chake ni pigo zito kwa familia yake,
Chama cha NCCR-Mageuzi, Chuo Kikuu cha Bagamoyo, Tume ya Mabadiliko ya Katiba
na kwa jamii nzima ya Watanzania.
"Kwa niaba ya Profesa Ibrahim Haruna Lipumba, Wajumbe wa
Baraza Kuu la Uongozi la CUF na Wanachama wote wa CUF na kwa niaba yangu
mwenyewe, tunatoa mkono wa tanzia kwa familia ya Marehemu, Mwenyekiti wa Taifa
wa NCCR-Mageuzi, Wajumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba na wafiwa wote,"
alisema.
CCM
yatoa pole
Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) umesikitishwa na
kifo cha Dkt. Mvungi na umeonya kuwa umaskini usifanye Watanzania kuwa chanzo
cha kuua watu wengine.
Akizungumza Dar es Salaam
jana Mkuu wa Idara ya Hamasa na Chipukizi wa UVCCM Taifa, Paul Makonda, alisema
wamepokea kwa masikitiko taarifa ya msiba huo.
"Umaskini wetu wa kipato, akili na mawazo, usiwe sababu ya
kuumizana na kugharimu maisha ya mtu kwani hata wale waliomvamia na kumjeruhi
huenda wamesukumwa na tamaa zao za kimaisha," alisema.
Polisi
yanasa mwingine
Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam linamshikilia mtu
mmoja anayetuhuniwa kuhusika katika tukio la mauaji ya marehemu Dkt.Sengondo
Mvungi.
Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam Kamishna wa Polisi Kanda,
Maalum Suleiman Kova alisema kuwa mtuhumiwa huyo alikamatwa juzi katika maeneo
ya Twiga Jangwani.
Kamishina Kova alisema kuwa; "mtuhumiwa alitambuliwa na
kukamatwa kisha kuhojiwa na Polisi na alikubali kuhusika katika tukio hilo na
askari waliongozana naye hadi nyumbani kwake Kiwalani Migombani ambapo alikutwa
na silaha ambayo ni bastola aina ya REVOLVER No.BDN 6111 pamoja na risasi 21 za
bastola hiyo ikiwa ni mali ya Dkt.Mvungi,"alisema Kova.
Pia katika upekuzi uliofanywa na Jeshi la Polisi katika chumba cha
mtuhumiwa vilipatikana baadhi ya vifaa vya mlipuko vya aina tofauti
vikiwemo,baruti aina ya Explgel, Tambi mbili ambazo ni viwashio vya baruti
pamoja na mlipuko.
Aliongeza kuwa mtuhumiwa alipohojiwa
kuhusu umiliki wa silaha hiyo alikiri kuwa hana kibali cha kumiliki silaha.
Alisema silaha hiyo ni miongoni mwa vitu vilivyoibwa kwa Dkt. Mvungi.
No comments:
Post a Comment