01 October 2013

YANGA 'YAIANGUKIA' SERIKALI


Na Fatuma Rashid

  Klabu ya Yanga imeiomba Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi pamoja na Manispaa ya Ilala, kujibu barua yao kuhusu kuomba eneo la nyongeza ili kukamilisha azma yao kujenga uwanja ambao utajulikana kwa jina la Jangwani City utakaokuwa na miundombinu yote
.  Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Mwenyekiti wa Kamati ya uwanja huo, Francis Kifukwe alisema barua ya kuomba eneo la nyongeza iliandikwa Desemba 12 mwaka jana, lakini mpaka sasa bado hawajapata jibu.

   Kifukwe alisema mpango wao katika ujenzi wa uwanja wa kisasa wa Yanga ni kuboresha mandhari nzima ya Jangwani kwa kukuza mazingira na miundombinu.

 "Tunahitaji eneo hili liwe na sura ya kibiashara na kitalii, ambapo tutahitaji kudhibiti mafuriko ambapo pia tutajaza udongo (kuweka tuta kubwa), upandaji miti, bustani za kubarizi na kuboresha mifereji ya maji taka," alisema.

  Alisema kutokana na kukua kwa jiji na katika hali ya kutaka klabu iwe na vitegauchumi, wameonelea ni vizuri kama ingekuwa na uwanja wa mpira wa kisasa utakaochukua watazamaji elfu 40.

  Aliongeza kuwa pia kutakuwa hosteli kwa ajili ya wachezaji, uwanja wa mazoezi, eneo la kuegesha magari, hoteli na sehemu ya makazi, ukumbi wa mikutano, ofisi, benki, zahanati ya wachezaji, supermarket na sehemu za kujipumzisha.

  Aliongeza kuwa mara baada ya azma hii kukamilika eneo hili litafahamika kama 'Jangwani City' na kufanya wakazi wa Jangwani na maeneo ya jirani wasiende maeneo ya mbali kutafuta huduma muhimu.

  Kifukwe alisema makubaliano ya awali yalisainiwa Novemba 23, mwaka jana ambapo inatakiwa kuwa na eneo la kutosheleza malengo ya mradi, kupata ushauri, michoro pamoja na mkandarasi mzuri wa miradi pamoja na kutenga fedha za kukamilisha usanifu na ujenzi wa miradi.

  Hivi sasa klabu hiyo ina kiwanja chenye ukubwa wa hekta 3.59 katika eneo lao la Jangwani ambapo kiwanja hicho kina hatimiliki kwa miaka 99 kuanzia mwaka 1972.

  Katika eneo hilo, klabu ilifanikiwa kujenga Uwanja wa Kaunda na jengo la klabu lenye ghorofa tatu. Jengo hili lilijengwa kwa ufadhili wa Rais wa kwanza wa Zanzibar, hayati Abeid Amani Karume, pamoja na michango ya wanachama na wapenzi wa klabu hiyo.

No comments:

Post a Comment