09 October 2013

MABASI YAGOMA KWA SAA SITA



Penina Malundo na Revina John
  Madereva wa mabasi yaendayo mikoani na nchi jirani katika Kituo cha Ubungo, jijini Dar es Salaam jana yamegoma kwa takriban saa sita wakishinikiza Serikali kutowatoza faini ya asilimia tano ya uzito unaozidi kwenye magari yao yanapopimwa kwenye mizani.

Mgomo huo ulioanza saa 12 asubuhi ulisababisha adha kubwa kwa abiria, huku madereva hao wakiwa wameshikilia msimamo wa kutoanza safari pasipo mwafaka kupatikana kati ya Chama cha Wamiliki wa Mabasi Tanzania (TABOA) na Serikali.
Dai jingine ni kuitaka Serikali kusitisha utaratibu wa kupima mabasi kwa madai kwamba mizani hiyo imekuwa ikitofautiana vipimo kutoka kituo kimoja hadi kingine.
Abiria waliokuwa wasafiri na mabasi hayo walilazimika kusubiri hadi saa sita mchana ambapo magari ya kwanza yalianza kuondoka Ubungo badala ya saa 12 asubuhi baada ya Serikali kuingilia kati.
  Mgomo wa madereva hao wa mabasi ulionekana kuzidiwa nguvu kutokana na wenye kampuni za magari hayo kukatisha tiketi kwa abiria wakati wakijua kwamba hawatawasafirisha.
  Abiria wengi walihoji sababu za wenye mabasi hayo kuchukua fedha zao za tiketi wakati wakijua hakutakuwa na safari.Usafiri wa mabasi kutoka Ubungo ulianza saa sita mchana baada ya kufikia mwafaka wa awali kati ya viongozi wa SUMATRA, Polisi na TABOA.
  Wenye mabasi hayo waliamua kuanza safari jana baada ya Serikali kukubaliana nao kuwa siku ya jana mabasi hayo hayatapimwa uzito kwenye mizani.Hata hivyo, waliendelea kusisitiza kuwa leo hawatasafirisha abiria wala kukatisha tiketi iwapo mwafaka hautakuwa umepatikana baina ya Serikali na TABOA.
  Akizungumza na gazeti hili Mjumbe wa Kamati Kuu ya TABOA, Rajabu Kasimu, alisema madai yao ni muda mrefu, lakini kutokana na kutopatiwa ufumbuzi ndiyo maana wameamua kugoma.
  “Tulitoa tangazo la mgomo leo (jana) kwa takriban siku nne ziliziopita, lakini tulikutana na Waziri Mkuu (Mizengo Pinda) akatuambia tusitishe mgomo wakati ufumbuzi ukitafutwa, lakini hadi juzi hatukuona utekelezaji wowote ndiyo maana tumefikia hatua hii," alisema Kasimu.
  Alisema kamati yao ilikutana na baadhi ya viongozi wa SUMATRA pamoja na Jeshi la Polisi ili kutafuta ufumbuzi, ndio maana wameamua kuanza safari kwa jana kwa sharti kuwa hakuna mabasi hayo kupimwa.
  Kwa Upande wake Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani, Mohammed Mpinga, aliagiza mabasi yaliyogoma kuanza safari mara moja na wale watakaokaidi watachukuliwa hatua ikiwa ni pamoja na kufutiwa leseni zao.
“Nimesema kuanzia sasa mabasi yaondoke na yale yatakayokaidi agizo langu tumekubaliana na wenzetu wa SUMATRA kuwachukulia hatua za kisheria ikiwa ni pamoja na kuwafutia leseni,” alisema Mpinga.
  Ofisa wa Chama cha Kutetea Abiria (CHAKUA) Gervas Rutaguzinda, alisema amesikitishwa na kitendo cha mabasi hayo kugoma na kugeuza abiria kuwa mateka. Meneja Leseni wa SUMATRA, Leo Ngowi, aliwataka madereva kusitisha mgomo huo na kuendelea kutoa huduma kwa abiria kama awali wakati suala hilo likitafutiwa ufumbuzi.
  Akizungumza na gazeti hili, Msemaji wa Wizara ya Ujenzi, Martin Ntemo, alisema sheria bado iko pale pale haijabadilishwa. Alisema chanzo cha malalamiko hayo ni kufukuzwa karibu asilimia 85 ya wafanyakazi kwenye mizani ambao walikuwa wamezoeana na wafanyabiashara. “Sasa hivi wafanyabiashara wanapata shida kuzoeana na wafanyakazi wapya kwenye mizani ndiyo maana wanalalamika,” alisema

No comments:

Post a Comment