01 October 2013

MAANDAMANO DAR KUPINGA MSWADA



   Muungano wa vyama vitatu vya siasa nchini NCCR-Mageuzi, Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) na Chama cha Wananchi (CUF) umeandaa maandamano makubwa ya kupinga kupitishwa kwa Mswada wa Sheria ya Marekebisho ya Mabadiliko ya Katiba wa mwaka 2013, anaripoti Darlin Said.

Mswada huo ulipitishwa na Bunge Mjini Dodoma hivi karibuni lakini wabunge wa vyama hivyo, walisimama bungeni na kupinga usipitishwe wakidai unatakiwa kufanyiwa marekebisho.
Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Mkurugenzi wa Mawasiliano na Uenezi wa CHADEMA, Bw. Bw. John Mnyika ambaye pia ni Mbunge wa Ubungo, alisema maandamano hayo ni haki yao ya msingi.
Alisema maandamano hayo yamepangwa kufanyika Oktoba 10 mwaka huu yakianzia Dar es Salaam na kuendelea katika mikoa mbalimbali nchini ili kupeleka ujumbe kwa wananchi.
“Hatutarudi nyuma na msimamo huu wa kufanya maandamano labda serikali iseme Rais Jakaya Kikwete hatasaini mswada huu kwani kuna kauli zinazoashiria tusiyafanye bali tujadiliane.
“Kama yakizuiwa kwa kigezo cha kutii amri bila shuruti hatuwezi kukubali, tutayafanya kwa sababu kila tunapoomba maandamano tunakatazwa,”alisema Bw. Mnyika.
   Aliongeza kuwa, kamati za ufundi za vyama hivyo, tayari zimeanza kutoa maelekezo mikoani na kuiomba Tume ya Mabadiliko ya Katiba, ijitokeze na kuelezea vifungu vyenye kasoro ambavyo wanavipigia kelele ili vibadilishwe.
  “Waziri wa Katiba na Sheria, Bw. Mathias Chikawe, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Uhusiano na Uratibu, Bw. Steven Wassira na Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Bi. Sophia Simba waache kumtisha Rais Kikwete na wananchi.
 “Chikawe anaposema kama rais hatasaini mswada huo anaweza kuingia katika mgogoro na hatimaye Bunge kuvunjika si ya kweli bali ni kuwapotosha wananchi, kama wana hofu wajiuzulu na kupisha watu wengine kushika nafasi zao,” alisema.
  Kwa upande wake, Mkurugenzi na Mawasiliano wa CUF, Bw. Abdul Kambaya, alisema hadi sasa Serikali ya Muungano na ile ya Mapinduzi Zanzibar, zinatambua kama kweli mswada huo haujakamilika kutokana na kasoro zilizopo.
  Majira lilipozungumza na Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Kamishna Suleiman Kova ili kujua kama maandamano hayo yamepata kibali alisema, hadi jana hakuwa amepata taarifa na wakizipata, watachunguza madai yao na kuangalia hoja zao kama wana jipya.

No comments:

Post a Comment