22 October 2013

DKT. SHEIN AVUNJA UKIMYA WA KATIBA

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Ali Mohamed Shein ambaye pianiMakamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Zanzibar, akifungua semina ya sikunneya watendaji na viongozi wa chama hicho ngazi ya wilaya na mikoa Mjini Dodoma jana

  • ASEMA CCM HAINA NIA YA KUHODHI MCHAKATO
  • ATOA AGIZO ZITO KWA MAKATIBU WILAYA, MIKOA
Na Elizabeth Joseph,Dodoma
  Chama Cha Mapinduzi ( C C M ) , k i m e s e m a hakijahodhi wala hakina nia ya kuhodhi mchakato wa Mabadiliko ya Katiba unaoendelea kama inavyosemwa na baadhi ya vikundi.
  Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar ambaye pia ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Ali Mohamed Shein, aliyasema hayo Mjini Dodoma jana wakati akifungua semina ya siku nne ya watendaji na viongozi wa CCM ngazi za wilaya na mikoa nchini.

Alisema kilichofanywa na CCM katika mchakato huo ni kutoa maoni kama ilivyoelekezwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba na si vinginevyo.

Aliongeza kuwa, baadhi ya watu wanasambaza maneno ya uzushi wakidai CCM inafanya hivyo kutokana na hofu ya kushindwa katika Uchaguzi Mkuu 2015 akiwafananisha na mfa maji ambaye haachi kutapatapa.

“Hayo ni mawazo ya mfa maji ambaye haachi kutapatapa. CCM haina nia hiyo wala hatuna hofu,” alisema Dkt. Shein na kusisitiza kuwa, chama hicho kilitoa maoni yake kama ilivyoelekeza tume wakitarajia vyama vingine navyo vingefanya hivyo.

Alisema katika mapendekezo yao ambayo yaliwasilishwa kwa tume hiyo, yamo yaliyotofautiana na yale yaliyomo katika rasimu, lakini CCM imefanya hivyo kutokana na dhamira yake ya kweli kuhakikisha nchi inapata Katiba Mpya yenye kukidhi mahitaji ya Watanzania wote.

“CCM itaheshimu maoni ya Watanzania kupitia kura ya maoni wakati ukifika...sisi hatujawahi kutamka na kudai maoni yetu ndio yachukuliwe na Tume ya Mabadiliko ya Katiba,” alisema.

Aliwataka watendaji hao kufuatilia kwa makini mafunzo ambayo watapewa ambapo mada 12 zitawasilishwa zikiwemo za maandalizi ya uchaguzi ili kuwajengea uwezo wa kiuongozi na kiutendaji waweze kutekeleza majukumu yao ipasavyo.

“Taratibu za kiutawala ni kwamba, Makatibu kazi yenu ni utendaji na kutoa ushauri wa kitaalamu kwenye vikao vyenu. Haipendezi na haileti sura nzuri kama shutuma za kuvuruga mchakato wa uchaguzi kwenye mikoa na wilaya zielekezwe kwenu.

 “Msijihusishe na makundi yenye nia ya kugombea nafasi mbalimbali za uongozi kwani muda wa kufanya hivyo bado haujafika...muwe nao kwa kuwa ni wanachama wenzetu katika chama lakini si kushirikiana nao katika nia yao ya kugombea,” alisema Dkt. Shein.

  Dkt. Shein alitumia fursa hiyo kusisitiza suala la maadili katika uongozi na utumishi wa chama akisema kuwa, kiongozi wa CCM lazima awe kioo cha uadilifu mbele ya umma.

 “Kiongozi wa CCM popote alipo, lazima awe mfano wa mtu mwema mwenye kufuata maadili, uadilifu, maelekezo ya Sera za chama chetu na kuzingatia sheria za nchi,” alisema.

  Alitoa wito kwa viongozi na watendaji wa CCM ambao wamekuwa wakifanya vitendo kinyume na maadili na uadilifu, wajirekebishe vinginevyo waachie ngazi.

  Alisisitiza uadilifu, uaminifu na nidhamu ni mambo muhimu katika kufanikisha ushindi wa chama chao ambacho hakiwezi kuwavumilia watu wanaoharibu taswira ya chama mbele ya jamii.

  Awali, akimkaribisha Makamu Mwenyekiti kuyafungua mafunzo hayo, Katibu Mkuu wa CCM, Bw. Abdulrahman Kinana, alisema miongoni mwa malengo ya mafunzo hayo ni kuimarisha chama hasa ngazi ya wilaya, matawi na mashina.

  Lengo jingine ni kuwajengea uwezo wa kiuongozi na kiutendaji watendaji hao ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi na weledi zaidi ambapo mafunzo hayo yatawapa fursa watendaji hao kujadiliana na kushauriana namna ya uendeshaji shughuli za chama katika mazingira ya sasa.
 

No comments:

Post a Comment