22 October 2013

WAFUASI WA PONDA WAACHIWA

  • MAHAKAMA KUU YABAINI KASORO ZA KISHERIA

 Na Grace Ndossa

  Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, imewaachia huru wafuasi 52 wa Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu, Shekhe Ponda Issa Ponda, waliokuwa wakikabiliwa mashtaka matatu.


  Hukumu hiyo ilitolewa Dar es Salaam jana na Jaji Salvatory Bongole ambaye alisema makosa yaliyowatia hatiani washtakiwa hao adhabu yake ilikuwa kifungo cha miezi mitatu gerezani au kulipa faini ya sh. 50,000 kila mmoja.

  Alisema kosa la kwanza ambalo ni kula njama halikuwa sahihi, hivyo adhabu ya kutumikia kifungo cha mwaka mmoja gerezani aliifuta.

  Aliongeza kuwa, kosa la pili na tatu anakubali kutiwa hatiani kwa washtakiwa, lakini alibadilisha adhabu ya kosa hilo inayowataka washtakiwa kukaa gerezani mwaka mmoja badala yake watakaa miezi mitatu gerezani au kulipa faini.

  Hata hivyo, Jaji Bongole alisema makosa yaliyowatia hatiani washtakiwa hao ni kula njama, kufanya mikusanyiko isiyo halali na kukaidi amri iliyotolewa na Jeshi la Polisi juu ya zuio la kutofanya maandamano.

  Alisema kifungu cha 384 kinaeleza kosa la kula njama na kuwatia hatiani, adhabu yake haikuwa sahihi. “Mlipewa adhabu mbili katika kosa moja, kula njama pamoja na kuiba.

 “Mlitiwa hatiani katika kosa la kuiba hivyo kosa la kula njama linakufa lakini mlipewa adhabu kwa makosa yote mawili...adhabu mliyopewa haikuwa sahihi,” alisema Jaji Bongole.

  Aliongeza kuwa, kosa la pili baada ya kupata ushahidi ameona upande wa Jamhuri ulithibitisha washtakiwa waliandamana wakati wakipinga amri ya Jeshi la Polisi.

 “Nakubaliana na umauzi ulitolewa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu ya kuwatia hatiani kwa kosa la pili na tatu la kukaidi amri iliyotolewa na Jeshi la Polisi kutoandamana.

 “Wakili wa washtakiwa, Mohamed Tibanyendera, alisema baada ya Mahakama ya Kisutu kuwatia hatiani, ilipaswa kuzingatia sheria ya kupunguziwa adhabu hiyo,” alisema Jaji Bongole.

  Alisema amefuatilia mwenendo wa kesi hiyo kwa makini hivyo anakubaliana na upande wa utetezi kuwa sheria ya kupunguziwa adhabu washtakiwa hao haikutiliwa maanani, adhabu ya kifungo haikufuata kifungu cha 46 cha Sheria za Polisi.

  Washtakiwa hao walihukumiwa kwenda jela Machi 21 mwaka huu ambapo hadi jana, walikuwa wamekaa gerezani kwa zaidi ya miezi saba, hivyo mahakama iliwaachia huru washtakiwa wote.

   Awali washtakiwa hao walitiwa hatiani katika makosa matatu ambayo kila moja adhabu yake ni kukaa gerezani mwaka mmoja na adhabu zote zilitakiwa kwenda kwa pamoja.

No comments:

Post a Comment