10 September 2013

WINGU DECI



  •  HATIMA YA WALIOPANDA  FEDHA SAS NJIA PANDA
  • DPP AKATA RUFAA,APINGA AMRI YA MAHAKAMA


 Na Rachel Balama
MKURUGENZI wa Mashtaka nchini (DPP), amewasilisha kusudio la kukata rufaa hukumu iliyotolewa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam dhidi ya vigogo wa Kampuni ya Development Entrepreneurship for Community Initiative (DECI).

Kampuni hiyo ilikuwa ikiendesha na kusimamia mchezo wa upatu ambapo taarifa ya kusudio la kukata rufaa, iliwasilishwa katika mahakama hiyo Agosti 23 mwaka huu.
Pamoja na mambo mengine, katika kusudio hilo DPP anapinga amri iliyotolewa na mahakama hiyo kuitaka Serikali pamoja na Benki Kuu ya Tanzania (BoT), ifanye utaratibu wa kurudisha fedha zilizopandwa na wanachama wa kampuni hiyo.
Wanachama hao ni wale watakaoonesha uthibitisho wa kupanda fedha zao DECI ambapo DPP anataka mahakama itamke wazi na kutoa maelekezi ni nani anayestahili kurejesha fedha hizo kwa wanachama hao.
Katika hukumu iliyotolewa na mahakama hiyo Agosti 19 mwaka huu, mahakama iliwahukumu vigogo wanne kati ya watano kifungo cha miaka mitatu jela au kulipa faini ya sh. milioni 21 kila mmoja.
Hukumu hiyo ilisomwa na Hakimu Aloyce Katemana kwa niaba ya Hakimu Stuwart Sanga aliyekuwa akisikiliza kesi hiyo na kudai kuwa, upande wa mashtaka umeweza kuthibitisha mashtaka yaliyokuwa yakiwakabili washtakiwa na kuwatia hatiani.
Hakimu Katemana alisema, pamoja na hukumu hiyo Serikali ifanye mchanganuo wa mali za DECI ambazo inazishikilia kwa kuwa zipo mali ambazo zinashikiliwa lakini ni za watu wengine.
Washtakiwa waliotiwa hatiani katika kesi hiyo ni Jackson Mtares, Dominick Kigendi, Timotheo Ole Loitignye na Samwel Sifael Mtares ambapo mshtakiwa Arbogast Kapilimba aliachiwa huru baada ya mahakama kushindwa kumtia hatiani.
Katika kesi ya msingi, washtakiwa hao wanakabiliwa na
mashtaka mawili ambayo ni kuendesha na kusimamia mradi wa upatu kinyume na kifungu 111A(1,3) cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu Sura ya 16.
Ilidaiwa kuwa, kati ya mwaka 2007 na Machi 2009, katika Makao Makuu ya DECI, yaliyopo Mabibo Mwisho, Dar es Salaam, washtakiwa waliendesha na kusimamia mradi wa upatu katika sehemu tofauti nchini kwa ahadi ya kuwapa wanachama wake fedha zaidi.
Shtaka la pili ni kupokea amana za umma bila kuwa na leseni kinyume na kifungu cha 6(1,2) cha Sheria ya Mabenki na Taasisi za Fedha namba 5 ya mwaka 2006 na kwamba washtakiwa wote katika kipindi hicho, wakiwa kwenye Ofisi za DECI, walipokea amana kutoka kwa umma bila leseni.
DECI iliwanufaisha watu wengi hasa waliojiunga mwanzoni na badaye kuibuka malumbano kati yao, Serikali na wanachama waliopinga kusitishwa kwa shughuli za taasisi hiyo.
Kusimamishwa kwa shughuli za DECI, kulitokana na uamuzi wa BoT kutoa taarifa ya kuwahadharisha Watanzania waliojiunga na upatu huo kuwa taasisi hiyo haiko kisheria na wanaweza kupoteza fedha walizopanda.
Upandaji mbegu katika taasisi hiyo, ulisitishwa baada ya Serikali kusimamisha akaunti za taasisi hiyo hadi uchunguzi utakapokamilika na kusababisha uvunjifu wa amani kwa wanachama wa DECI na viongozi wa taasisi hiyo.
Baadhi ya wanachama waliamua kuchukua sheria mkononi kwa kuvunja vioo vya magari ya viongozi, wakitaka warejeshwe fedha zao.
Katika kesi hiyo, upande wa Jamhuri ulikuwa unawakilishwa na Wakili, Prosper Mwangamila na Justus Mulokozi, ambapo washtakiwa hao walikuwa wanatetewa na mawakili wa kujitegemea Hudson Ndusyepo na Onesmo Kyauke.
Wakili wa DECI
Siku moja baada ya mahakama hiyo kutoa hukumu, Majira lilizungumza na Wakili wa washtakiwa Bw. Ndusyepo, ambaye alisema kuwa, mahakama hiyo imeshindwa kusimamia vizuri sheria iliyowatia hatiani wateja wake na kuwaacha wanachama.
Alisema yeye hapingani na hukumu iliyotolewa na mahakama lakini sheria ya adhabu kifungu cha 171 (A), kama ilivyorekebishwa na sheria namba 8 ya mwaka 2006, haikutekelezwa ipasavyo.
Bw. Ndusyepo alisema sheria hiyo pia inawatia hatiani wanachama wote waliopanda fedha zao DECI kwa kushiriki upatu, hivyo mahakama inapotoa amri kwa Serikali irudishe fedha za wanachama hao ni sawa na kuwazawadia wahalifu.
Aliongeza kuwa, kama sheria hiyo imetumika kuwatia hatiani wateja wake, haikupaswa kuwaacha wanachama ambao kwa mujibu wa sheria nao walipaswa kutiwa hatiani kwani kitendo cha kushiriki upatu kinakatazwa na sheria hiyo.
“Wanachama wa DECI nao ni wahalifu kwa mujibu wa sheria hii hivyo walipaswa kutiwa hatiani kwa kujihusisha na upatu ambao upo kinyume cha sheria.
“Haikuwa rahisi kuwakusanya wanachama wote na kuwaunganisha katika hati ya mashtaka moja ndio maana ilikuwa rahisi kuwashtaki Wakurugenzi kwa niaba ya wote,” alisema.
Aliongeza kuwa, amri iliyotolewa na mahakama hiyo kutaka wanachama wa DECI warudishiwe fedha zao inaondoa dhana ya Bunge kutunga sheria inayozuia mchezo wa upatu.

No comments:

Post a Comment