05 September 2013

WERUWERU YAONGOZA WIZI WA MAJI



Na Florah Temba, Moshi
KIJIJI cha Chekereni Weruweru Wi l a y a y a Mo s h i mk o a n i Kilimanjaro, kimetajwa kuongoza kwa wizi wa maji, hali ambayo imekuwa ikiisababishia Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Mjini Moshi (MUWSA) kupata hasara
.Hayo yalibainishwa jana na Ofisa Uhusiano wa MUWSA, Dorah Kilo wakati wa operesheni ya kuwabaini wananchi wanaojiunganishia maji kinyume cha sheria na taratibu, jambo ambalo limekuwa likiisababishia mamlaka kupata hasara kubwa.
Kilo alisema kwa siku Mamlaka hiyo huzalisha mita za ujazo 1,200 za maji katika kijiji hicho lakini asilimia 80 ya maji hayo hupotea, kutokana na baadhi ya wananchi kujiunganishia maji kinyume cha Sheria na taratibu.
"Kumekuwepo na upotevu mkubwa wa maji katika kijiji hiki, kwani kwa siku tumekuwa tukizalisha maji mita za ujazo 1,200, lakini asilimia 80 ya maji hayo hupotea, na upotevu huu husababishwa na watu kujiunganishia maji kinyume cha sheria," alisema.Alifafanua kuwa Mamlaka hiyo kwa sasa hupoteza asilimia 28 ya maji yanayozalishwa ambapo asilimia 80 ya upotevu huo inatoka katika kijiji cha Chekereni Weruweru.
Alisema katika operesheni waliyoifanya kwenye Kijiji hicho changamoto kubwa waliyokutana nayo ni wananchi kujiunganishia maji kinyume cha sheria, jambo ambalo limekuwa likisababisha kuendelea kuwepo kwa upotevu mkubwa wa maji.
"Katika operesheni tuliyoifanya, tumekutana na changamoto kubwa ya mkazi mmoja kujiunganishia maji isivyo halali na amechimba kisima, lakini pia amepandisha maji kwenye tanki kwa kutumia mota jambo ambalo ni kinyume cha sheria, kwa kweli hii ni hujuma kubwa kwa Mamlaka na serikali kwa ujumla," alisema Kilo.Kutokana na hali hiyo mamlaka hiyo ilimtaka msimamizi wa eneo hilo kuhakikisha kiwango cha upotevu wa maji kinapungua ifikapo mwishoni mwa mwezi Septemba mwaka huu.
Aidha Dorah alitumia pia nafasi hiyo kuwaasa wakazi wa Kijiji cha Chekereni Weruweru, kuacha mara moja tabia ya kujiunganishia maji kinyume cha sheria na kwamba kwa yeyote atakayebainika atachukuliwa hatua kali za kisheria ikiwa ni pamoja na kusitishiwa huduma ya maji.
"Niwatahadharishe wananchi wa eneo hili, waache haraka sana kujiunganishia maji kinyume cha sheria, kwani hatua ya kwanza tutakayoichukua kwa mtu atakayebainika kufanya hivyo, ni kumkatia maji kwa mujibu wa sheria na kumtaka alipe gharama ambazo zilipotea kutokana na wizi wa maji aliokuwa akiufanya," alisema.
Akizungumza Mwenyekiti wa Kitongoji cha Katanini Kijiji cha Chekereni Weruweru, Yahaya Salum aliwataka wananchi kutoa ushirikiano kwa mamlaka ya majisafi na usafi wa mazingira MUWSA, na kuhakikisha wanawafichua wale wote ambao wamekuwa wakijiunganishia maji kinyume cha Sheria ili hatua kali za kisheria ziweze kuchukuliwa dhidi yao.

No comments:

Post a Comment