05 September 2013

WAZEE WAUPINGA UONGOZI YANGA



Na Hussein Ally
BAADA ya uongozi kufanya mabadiliko ya sekretarieti ya klabu hiyo, Baraza la Wazee limeibuka na kupinga mabadiliko hayo.Yanga imemuengua Katibu, Lawrence Mwalusako na kumwajiri raia wa Kenya, Patrick Naggi, lakini Baraza la Wazee wamesema hawatambui mabadiliko hayo.

Patrick aliibuka katika makao makuu ya Yanga jana na kuwafahamisha kuwa amekuja kufanya kazi ya Katibu Mkuu wa klabu hiyo, baada ya kuomba nafasi hiyo kupitia kwa kiongozi ambaye hakutaka kumtaja.Baraza la wazee lilishtuka kusikia ujio wa Katibu huyo na kushangaa mwenendo mzima uliofanyika, kwani katika katiba ya Yanga hakuna kitu kinachofanyika bila ya baraza hilo kutambulishwa.
Wazee hao baada ya kuona hali hiyo jana waliamua kutoa tamko kupitia kwa Katibu wa Baraza la Wazee, Yahaya Akilimali ambaye alisema wao kama wazee hawamtambui katibu huyo na hawamtaki.Akilimali alisema, shughuli zote za uongozi ndani ya Klabu ya Yanga kwa mujibu wa katiba zinafanywa na mwanachama wa Yanga kwa hiyo katibu huyo hajulikani ametokea tawi gani.
"Kwa niaba ya Mwenyekiti wa Baraza la Wazee, natoa tamko rasmi sisi wazee wa Yanga hatumtaki katibu huyo mpya na tunataka mara moja arudi kwao," alisema.Alisema kuna mambo makuu matatu, ambayo wao hawamtaki katibu huyo kwanza wazee wa klabu hiyo hawajafahamishwa, pili Kamati ya Utendaji ya klabu hiyo haina taarifa naye, tatu makatibu na wenyeviti wa Mkoa wa Dar es Salaam hawajui lolote.
Hata hivyo katibu huyo mpya alipoulizwa na wazee nani amemleta katika klabu hiyo, alikataa kusema na kumuona huenda akawa tapeli anataka kuitapeli Yanga.Wazee hao walisema, Yanga si jalala la kila mtu anayetaka kuongoza anakubaliwa kwa hiyo wamewataka viongozi wenye lengo baya na Yanga kuacha mara moja tabia hiyo.
Walisema, kitu chochote kinachofanyika ndani ya Yanga huwa na taratibu, Mwenyekiti huwaita wazee na kuwashauri baadaye ndiyo linatolewa tamko kama ilivyofanyika katika malumbano juu ya TV Azam.Yanga mpaka sasa bado haijampata Katibu Mkuu, kwa sasa Mwalusako ndiye anayekaimu nafasi hiyo baada ya Mwesigwa Selestine kuenguliwa mwaka jana.

No comments:

Post a Comment