05 September 2013

BOT YATOA LESENI KWA KAMPUNI MPYA



Na Salim Nyomolelo
KAMPUNI inayohusika na masuala ya mikopo ya Dun & Bradstreet Credit Bureau imeahidi kuongeza ufanisi katika utendaji wa shughuli zake baada ya kupokea leseni ya uendeshaji kutoka Benki Kuu ya Tanzania (BoT).

Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, Ofisa Mtendaji Mkuu wa kampuni hiyo, Miguel Llenas alisema hatua hiyo itaiwezesha kampuni yake kutoa huduma za utunzaji wa kumbukumbu za mikopo.
Sambamba na kutoa mikopo kwa ufanisi wa juu na hivyo kuleta manufaa kwa wateja wake hapa nchini.
" K u t o l e w a k w a l e s e n i kumefungua ukurasa mpya kwa wadau wote wenye nia ya dhati ya kuona uchumi unaoimarika na wenye nguvu zaidi. Mfumo huu umeipa sekta ya fedha fursa ya kuboresha huduma za mikopo kwa urahisi," alisema Llenas.
Alisema, ushirikiano wanaoupata kutoka BoT wakiwemo wadau wengine, utasaidia mfumo huo wa kumbukumbu za mikopo na wakopaji ulioanzishwa na Benki Kuu kuleta manufaa makubwa kwa Taifa zaidi katika kukuza uchumi.
"Tunafuraha kubwa kuanza rasmi uendeshaji wa huduma hii nchini Tanzania, matumaini yetu tutaweza kujenga na kutoa huduma bora na yenye thamani kwa wadau wote, pia kupitia hatua hii benki za Tanzania zitaongeza kasi ya huduma zake za mikopo, kupunguza gharama za uendeshaji na kuwa na taarifa sahihi za utendaji wake," aliongeza Llenas.  

No comments:

Post a Comment