09 September 2013

UZALISHAJI SUKARI NCHINI KUONGEZEKA



Na Florah Temba, Moshi
KIWANDA cha sukari cha TPC kilichopo Wilaya ya Moshi mkoani Kilimanjaro kinatarajia kuongeza uzalishaji wa sukari kutoka tani 92,000 zilizozalishwa kipindi cha mwaka 2012/2013, hadi kufikia tani 100,000 kwa kipindi cha mwaka huu 2013/2014.

Hayo yalibainishwa na Ofisa mtendaji mkuu na utawala wa kiwanda hicho, Jafary Ally wakati akizungumza na gazeti hili ofisini kwake kuhusiana na hali ya uzalishaji katika kiwanda hicho.
Jafary alisema uzalishaji wa sukari katika kiwanda hicho umekuwa ukiongezeka mwaka hadi mwaka na hivyo katika kipindi cha mwaka huu wanauhakika wa kuongeza uzalishaji kutoka tani 92,000 hadi kufikia tani 100,000.Alisema kiwanda hicho kwa siku huzalisha sukari tani 500 na kwamba bado wataendelea kuongeza nguvu za uzalishaji ili kufanikisha malengo ya Serikali ya kuinua uchumi kupitia viwanda.
"Wakati kiwanda hiki kimeanza kilikuwa kinazalisha sukari tani 36,000, uzalishaji huu umekuwa ukiongezeka mwaka hadi mwaka na kufikia tani 92,000 na mwaka huu tunatarajia kuongeza uzalishaji hadi kufikia tani 100,000, uzalishaji ambao haujawahi kutokea," alisema Jafary.
Alisema ongezeko la uzalishaji huo wa sukari,litatokana na uzalishaji mzuri wa miwa katika kipindi cha mwaka huu na kwamba hali hiyo itawawezesha kuvunja rekodi ya uzalishaji.Alisema katika kipindi cha mwaka huu waliweza kufuata kanuni za kilimo bora cha miwa ambacho kimeonesha mafanikio makubwa katika uzalishaji wa miwa.
Alisema ongezeko la uzalishaji huo linaweza kuwapa fursa ya kushika nafasi ya kwanza kwa uzalishaji Afrika, kutoka nafasi ya tatu ambayo walishika mwaka jana."Mbinu za uzalishaji huu mzuri wa miwa ni kufuata kanuni za kilimo bora cha miwa na hii inaweza kutufanya tushike nafasi ya kwanza Afrika kwa uzalishaji kwani hatujaongeza ukubwa wa ardhi na tulichofanya ni kuzingatia kanuni," alisema.

No comments:

Post a Comment