09 September 2013

'KATIBA MPYA ITAMKE ELIMU BURE KWA WALEMAVU'



TUME ya Mabadiliko ya Katiba imeundwa kwa mujibu wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba Sura ya 83 ambayo ina kazi ya kukusanya maoni ili kufanikisha kwa Katiba Mpya hapa chini.Tume hiyo yenye wajumbe 32 ikiongozwa na Mwenyekiti na Jaji Joseph Warioba imekuwa ikifanya jitihada za kuhakikisha kuwa wananchi wanatoa maoni yao pamoja na makundi maalumu ili yaingizwe kwenye Katiba mpya hususani baada ya kuchambua rasimu ya Katiba Mpya na kuona mambo yaliyosahaulika yanayogusa makundi hayo
.Makundi mbalimbali yalipata fursa ya kuchambua rasimu ya Katiba Mpya na kutoa mapendekezo yao kuhusiana na mambo wanayotaka yaongezwe, yaondolewe na mengine kubaki kama yalivyo, hii imefanyika ili kutoa haki pande zote.Kundi la walemavu na wanaoishi na virusi vya Ukimwi ni miongoni mwa makundi yaliyopata nafasi ya kutoa maoni yao ya kuchangia rasimu ya Katiba Mpya ambapo makundi hayo nayo yalipata fursa ya kuchangia maoni yao kama makundi maalumu.
Mwenyekiti wa Shirika la Kilimo la Walemavu Songea (SHIKIWASO) ambaye pia ni mlemavu wa viungo, Bw. Ally Kiponda anasema kuwa awali katika mabaraza ya Katiba makundi ya walemavu na wanaoishi na Virusi vya Ukimwi hayakupata fursa ya kuingia kwenye makundi ya kuchangia rasimu ya Katiba Mpya ambayo yalikuwa katika makundi ya wanawake, vijana na kundi la jiografia ambalo lilijumuisha makundi yote.
Anasema kuwa kwa ufadhili wa Shirika la Foundation for Civil Society (FCS) wao waliamua kuendesha Baraza la Katiba kwa Watu wanaoishi na Virusi vya Ukimwi (WAVVU) na walemavu ili kutoa fursa kwa makundi hayo nayo kutoa maoni yao ili yaingizwe kwenye Katiba Mpya hatua ambayo itaonesha makundi yote yamefikiwa.
Akichangia kwenye mkutano wa Baraza la Katiba uliofanyika kwenye Ukumbi wa Maktaba mjini Songea mmoja wa walemavu, Bw. Samwel Mapunda anapendekeza suala la walemavu kupata elimu bure kuanzia elimu ya awali hadi chuo kikuu.
Pia vifaa maalumu kama fimbo nyeupe liingizwe kwenye Katiba Mpya huku pia akisema katiba itamke haki ya kupata ajira kwa walemavu na kuwepo uwakilishi kwa wenye ulemavu kuanzia ngazi ya kitongoji hadi Taifa.
"Katiba pia itamke kuwa walemavu wapate huduma za afya bure na kutengewa eneo la kupata huduma hizo bure bila bughudha na pia wapatiwe vifaa vya kujimudu ili waweze kupata huduma nyingine muhimu kwa maisha yao na kuchangia pato la Taifa," anasema.
Akichangia kwenye mkutano huo mlemavu mwingine Bw. Christopher Mwamalili ametaka kuwepo na usawa wa masuala mbalimbali kwa walemavu na kwamba suala hilo liwepo kikatiba si kwa kuzungumzwa tu mdomoni.
Anasema kuwa kunatakiwa kuwepo kwa usawa wa viti vya wanawake vya uwakilishi bungeni lakini kundi la walemavu limekuwa na uwakilishi kwa kiasi kidogo sana.
Mchangiaji mwingine Bw.Kasim Mngwali ametaka a s a s i za kuwahudumia walemavu zisiwatumie walemavu kama mtaji na hivyo waachiwe walemavu wenyewe kuzishughulikia asasi hizo kwa ustawi wa walemavu na kuondokana na kuwa ombaomba.
Aidha mchangiaji mwingine ametaka walemavu wapate huduma za afya bure na suala hilo kuingizwa kwenye Katiba Mpya ambapo akichangia kuhusiana na watu wanaoishi na Virusi vya Ukimwi ametaka Katiba itamke kupata huduma za matibabu bure kwa watu wanaoishi na virusi vya Ukimwi.
Anapendekeza hukumu ya kifo ifutwe na badala yake kuwepo na kifungo cha maisha jela ili kutoa nafasi kwa mkosaji kujutia makosa yake akiwa gerezani badala ya kumhukumu kifo ambapo hata hivyo katika utoaji wa mapendekezo hayo wajumbe walitofautiana katika kipengele hicho ambapo wengine wametaka adhabu ya kifo ibaki kama ilivyo.
Pia wachangiaji katika mkutano huo wa Baraza la Katiba wametaka mawaziri wasiwe wabunge na kwamba wapewe nafasi hizo kwa kuzingatia taaluma zao ili kuleta ufanisi katika utendaji wa kazi ambapo akichangia katika hoja hiyo Bw.Selestine Mkomekwa ametaka Makatibu wakuu kwenye Wizara kuwajibika.
Kat ika Baraza hi lo suala lililochangiwa na wachangiaji wengi ni suala la Muungano huku wachangiaji wengi wakipendekeza kuwepo na Muungano wa Serikali tatu na kubainisha kuwa Muungano huo wa Serikali tatu utaondoa utata kwani rais wa Muungano atatatua kero zao kwa kuwa wamekuwa wakinyanyasika.
Akichangia hoja kuhusiana na Muungano, Mzee Daud Mtupa anasema kuwa nchi mbili Tanganyika na Zanzibar baada ya kupata huru Tanganyika ilijipeleka jumla kwenye muungano na kupotelea huko ambapo muungano wa sasa hauoneshi wameungana na nchi gani na kupendekeza kurejeshwa kwa Serikali ya Tanganyika.
"Mimi napendekeza Tanganyika irudi kisha tuungane na napendekeza Zanzibar kuwe na Waziri Mkuu na Tanganyika kuwepo Waziri Mkuu na kisha kuwepo na Rais wa Jamhuri ya Muungano ili kuondoa utata wa kiutawala," alisema.
Mchangiaji mwingine ambaye ni mlemavu wa viungo Bw. Mngwali anazungumza kwenye baraza hilo kuwa rasimu hiyo imekuja wakati mwafaka wa kudai Serikali ya Tanganyika ambapo anapendekeza kuwepo na Serikali tatu, Serikali ya Muungano, Tanganyika na Zanzibar na kwamba huenda akiwepo Rais wa Muungano atawajali Walemavu.
 Akichangia hoja kwenye mkutano huo Bw. Percival Bwanali kwa upande wake anasema kuwa kwa kuwepo na Muungano wa Serikali tatu kutaondoa utata wa Zanzibar kujiona kuwa wanaonewa na Tanganyika.
Anasema kuwa kutokana na utata wa muungano Wazanzibari wamekuwa wakidai nchi yao kwa asilimia 100 hivyo muungano wa Serikali tatu utaondoa utata huu uliopo na hivyo hakutakuwepo na malalamiko ya pande hizi mbili Tanganyika na Zanzibar.
Kwa upande wake mshiriki Bw. Kasim Lyanda anapendekeza kuwepo na Muungano wa Serikali tatu na kubainisha kuwa kuwepo kwa Muungano huo kutaleta Muungano halisi kwa kuwa itaonesha Tanganyika imeungana na Zanzibar tofauti na ilivyo sasa ambapo Serikali ya Tanganyika haipo.
Akichangia hoja kuhusiana na Muungano, Bw. Mnung'a S. Mnug'a anasema kuwa Tanganyika na Zanzibar ni nchi zilizo huru na hivyo zinaweza kuunda muungano wa Serikali tatu wenye rais mmoja na akapendekeza kuwepo na magavana katika nchi za Tanganyika na Zanzibar na kubaki na Rais mmoja wa Serikali ya Muungano.

No comments:

Post a Comment