09 September 2013

UVCCM WAPIGANIA MIKOPO YA VIJANA



 UMOJA wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) wilayani Korogwe, umewataka watendaji wa halmashauri kuweka utaratibu utakaowezesha vijana kupatiwa mikopo itakayotokana na fedha zilizotengwa na Serikali kiasi cha shilingi bilioni 6.1.

Mwenyekiti wa UVCCM wilayani Korogwe, Bendera Shekigenda alitoa ushauri huo mwishoni mwa wiki kwenye mkutano wa siku moja kwa Saccos ya vijana wa Korogwe vijijini ulioandaliwa kwa ajili ya kuwapatia mbinu vijana namna watakavyojiandaa na mikopo hiyo.
Mkutano huo uliohusisha vikundi 169 vya vijana wanaounda Saccos hiyo ambapo Shekigenda alisema ili waweze kunufaika na mikopo hiyo vijana wanatakiwa kuwa wabunifu wa miradi wakijitahidi kutumia rasilimali walizonazo na zilizowazunguka katika kuendesha miradi ya kujikwamua kiuchumi.
Alisema kwamba upatikanaji wa fedha hizo kama sehemu ya mikopo kwao kutoka kwa Serikali yao inahitaji ubunifu wa hali ya juu kuwawezesha kujikwamua kimaisha ambapo aliwasisitiza kuongeza ubunifu badala ya kufanya biashara zitakazofanana utaratibu ambao unaweza kuwakwamisha.
Mbali na kuyasema hayo, Shekigenda pia aliwashauri maofisa wa vijana kuwafikia vijana wote katika maeneo ya vijijini kuwaeleza juu ya fursa iliyopo lengo likiwa kuwawezesha kushiriki katika mchakato wa kujiunga na Saccos yao lengo likiwa kuwakwamua katika lindi la umaskini wa kipato kwa walio wengi.
Mwenyekiti huyo alisema utolewaji wa mikopo hiyo unawahusisha vijana wote bila ya kujali dini, itikadi za vyama vya siasa wala ukabila ambapo aliwahimiza wajumbe wa mkutano huo kuwa mabalozi wazuri kwa wenzao ambao hawakuweza kupata taarifa ili waweze kuungana nao.
Kuhusu vikwazo ambavyo vitajitokeza wakati wa mchakato wa upatikanaji wa mikopo, Shekigenda alisema kwamba ni vyema vijana watakaojihisi kukwama kutokana na kujitokeza kwa upungufu mbalimbali wakajitahidi kuonana na viongozi wao wakiwemo wale wa vijana ili kupatiwa ufumbuzi.
Katika mkutano huo uliofanyika katika ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Korogwe mkoani Tanga zaidi ya vijana 260 walihudhuria kutoka katika kata 12 ambapo walishiriki kuchangia rasimu ya katiba ya Saccos yao huku wakihimizwa kuwa kwenye vikundi vya watu kuanzia idadi ya watano hadi kumi

No comments:

Post a Comment