09 September 2013

UFUGAJI NYUKI KITAALAMU HUPUNGUZA UHARIBIFU MISITU



Lilian Justice
Mizinga ya nyuki ikionekana pichani ikiwa imetundikwa bila ya kuharibu mazingira. Picha na Lilian Justice
UHARIBIFU wa mazingira ni uzoroteshaji wa mazingira kwa njia ya kupunguza rasilimali kama vile hewa, maji na udongo.Kutokana na uharibifu wa mazingira unaojitokeza kila mara katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu imepelekea Serikali kupitia Bunge kuanza kutunga sheria au kuweka mkakati maalumu wa kuweza kuzuia uharibifu huo.

Uharibifu wa mazingira unaofanywa na binadamu kutokana na kutafuta mahitaji yake unaweza kudhibitiwa kwa njia mbalimbali kama kutakuwepo na ushirikiano mkubwa kati ya Serikali na taasisi binafsi zinazopambana na utunzaji wa mazingira kila wilaya na kila mkoa kwa elimu endelevu ya mazingira.
Katika Mkoa wa Morogoro kuna tatizo kubwa la uharibifu wa mazingira japokuwa kuna taasisi nyingi binafsi ikiwemo mashirika zinazopambana na changamoto hii inayochangia mabadiliko makubwa ya tabia nchi yanatokea mara kwa mara kutokana na ukosefu mkubwa wa elimu ya mazingira hasa katika Milima ya Uluguru.
Katika kuhakikisha changamoto hiyo inavaliwa njuga taasisi isiyo ya kiserikali ya Blesssing Group inayojishughulisha na ufugaji wa nyuki na samaki pasipo kuharibu mazingira imefanikiwa kwa kiasi kikubwa kutekeleza majukumu yake katika sehemu mbalimbali za Mkoa wa Morogoro za kuhimiza ufugaji salama ambao haugusi mazingira.
Aidha mwenyekiti wa asasi hiyo Aron Mlemi anaeleza kuwa malengo ya taasisi hiyo ni kuinua uchumi, maendeleo ya wananchi sambamba na Mkakati wa Taifa wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umaskini Tanzania (MKUKUTA) pamoja na utunzaji wa mazingira na misitu kwa kutoa elimu na upandaji wa miti sambamba na kutokata miti ovyo.
Anasema kuwa asasi yao inatoa mafunzo kwa ajili ya kujenga uelewa kwa jamii na wadau wakuu kushiriki katika ufugaji wa nyuki kitaalamu na utunzaji wa mazingira na kuhamasisha kila kijiji katika wilaya ya Mvomero kutenga maeneo maalum kwa kufanikisha mchakato huo.
Mlemi anafafanua kuwa kupitia mradi wa ufugaji wa nyuki kwa njia bora ya kisasa wamehamasisha kujenga uelewa kwa jamii kuonesha uthubutu kwani unasaidia katika suala zima la utunzaji wa mazingira na kuongeza kipato katika jamii wanazoishi.
Vilevile anaongeza kuwa kuanzisha na kuendeleza ufugaji wa nyuki kwa njia za kisasa wilayani Mvomero unazingatia utunzaji wa mazingira na unaochangia kikamilifu kwenye uchumi wa wafugaji pamoja na mradi huo.
Anataja malengo ya asasi kuwa ni kuhamasisha ufugaji wa samaki, kuhimiza matumizi bora ya ardhi, matumizi bora ya misitu na bionuwai, kuanzisha vitalu vya miti na mazao mengine rafiki wa mazingira na nyuki, kilimo kinachochochea utunzaji wa mazingira kuhimiza wafugaji wa nyuki kwamba ufugaji uwe wa kisasa na kuhimiza uzalishaji wenye tija katika jamii.
Anasema kuwa kuna tatizo kubwa sugu katika Wilaya Mvomero ya uchomaji wa misitu ovyo hasa nyakati za kiangazi, maeneo mengi ya milimani yanakuwa tayari yameshawashwa moto kutokana na shughuli za kilimo sababu kubwa ni kundi kubwa kuishi kwa kutegemea shughuli za uchomaji mkaa kama njia ya kujipatia kipato na hivyo kujikuta wanachangia kwa asilimia kubwa kuharibu mazingira.
Anasema kuwa asasi hiyo imejipanga kushirikiana na wadau mbalimbali wa maendeleo ikiwemo Serikali katika kuelimisha jamii umuhimu wa kutunza mazingira kwa kutambua miti na misitu ni rafiki kwa binadamu na zawadi ya asili na faida nyingine kama mbao, asali na anta, dawa za asili, malisho ya mifugo, hali ya hewa nzuri na yanzo vya maji.
Mwenyekiti huyo anasema kuwa kupita mradi wa ufugaji wa nyuki asasi hiyo inaamini kuwa pamoja na kuongeza pato la taifa na kaya kwa kiasi kikubwa pia inasaidia kulinda misitu na utunzaji wa mazingira kwa faida ya vizazi vilivyopo na vizazi vijavyo kwani mazingira mazuri ndiyo yatachangia kuwepo kwa huduma hizo muhimu ndani ya jamii.
Wafugaji wengi wa nyuki wakihamasishwa katika kila kijiji na kutenga maeneo wanajikuta wameingia katika utunzaji wa mazingira kwani bila miti huwezi kufuga nyuki na watakosa chakula kwani nyuki wanategemea kwa asilimia kubwa kupata vyakula vyao katika miti.
Katika mchakato mzima wa ufugaji wa nyuki hakuna mfugaji anayekubali shamba lake la mizinga likachomwa moto na jamii ikiwa na uelewa umuhimu wa misitu itasaidia katika kulinda na kutunza mazingira kwa kuwa wanaelewa tayari faida wanayoipata kutokana na kuweka mazingira katika hali ya usalama.
Anasema kuwa changamoto zinazojitokeza katika suala zima la ufugaji wa nyuki kwa njia za kisasa na utunzaji wa mazingira ni kutokuwa na elimu endelevu ya ufugaji wa nyuki kitaalamu kwa njia bora za kisasa badala ya ufugaji uliojengeka wa mizinga ya magome ya magogo ambao huchangia kwa asilimia kubwa uharibifu wa mazingira.
Anasema kuwa nyingine ni pamoja na asali kuuzwa kabla ya kuchakatwa wilayani Mvomero na mwingiliano mkubwa wa matumizi ya ardhi ambayo si rafiki kwa ufugaji nyuki kwa bora ya kisasa, nyuki kuhama kwa kukosa chakula kwa tatizo la uchomaji moto misitu ovyo, ukosefu wa vitendea kazi, ukosefu wa rasilimali fedha na mwamko mdogo katika ufugaji wa nyuki.
Kutokana na jitihada zinazofanywa na asasi, serikali wilayani Mvomero kupitia Mkuu wa Wilaya, Antony Mtaka wakati anazungumza na vikundi vinavyojihusisha na ufugaji wa nyuki na utunzaji mazingira kutoka Tarafa ya Turiani anasema kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na taasisi hiyo katika harakati za kuleta maendeleo hasa katika nyanja za utunzaji wa mazingira ambayo imekuwa kero kubwa kwa taifa.
Mtaka anabainisha kuwa mchango unafanywa na taasisi binafsi hasa zinazopambana na mazingira katika kuleta maendeleo ni mkubwa sana na Serikali inathamini sana mchango wao na watakuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha zinakabiliana na changamoto zinazoikabili jamii kwa nyakati taofuti.
“Sisi Serikali tutakuwa mstari wa mbele katika kutoa mchango wetu kwa taasisi binafsi hasa zile zinazopambana na utunzaji wa mazingira kwani uharibifu wa mazingira unachangia mabadiliko makubwa ya tabia ya nchi,” alisema Mtaka.
Anaeleza kuwa ufugaji wa nyuki hauna gharama kubwa ila kinachotakiwa ni mfugaji kuwa na elimu ya kutosha na kufuata mbinu sahihi za ufagaji kwa lengo la kupata mazao bora pasipo kuharibu mazingira kwa kuchomo moto misitu ya asili ambayo ni kivutio katika jamii.
Kwa upande wake Mratibu wa mradi wa ufugaji nyuki kwa njia za kisasa na utunzaji wa mazingira, Richard Haule, anasema kuwa asasi imejikita katika mradi wa ufugaji nyuki kama chanzo kikuu cha mapato na kushiriki kikamilifu vikundi ambao ni wadau wakuu wa maendeleo katika jamii kwa kadiri ya fursa kwa kufuga na kutunza mazingira kwa kushirikiana na Serikali kama mdau mkubwa wa maendeleo ya umma.
Haule anasema asasi inatoa elimu kwa jamii na kujenga uelewa kupitia vikundi mbalimbali vya kijamii kuamsha na kushirikisha kikamilifu katika mradi wa ufugaji wa nyuki kwa njia bora ya kisasa na utunzaji wa misitu ya kupandwa na misitu asili pia ufugaji wa samaki ikiwa ni jitihada za kupambana na umaskini katika jamii.
Naye mmoja wa wafugaji wa nyuki Katika Wilaya ya Mvomero, Msafiri Kimath anasema kuwa ufugaji wa nyuki unaweza kumkwamua mwananchi kiuchumi na kuweza kutatua changamoto mbalimbali za kimaisha ikiwemo kusomesha watoto ,ujenzi wa nyumba ya kuishi na hata kuweza kumudu gharama mbalimbali za matibabu kwa familia.
Kimath anasema kuwa ni vyema wananchi wakaachana na kasumba kuwa ufugaji wa nyuki hauna tija kwa maendeleo jambo ambalo si sahihi na badala yake wananchi wanaotaka kujikita katika ufugaji wa nyuki kuwasiliana na maafisa ugani ili waweze kuwapa elimu juu ya ufugaji bora wa kisasa wa nyuki.
Hivi karibuni Waziri Mkuu Mizengo Pinda alitoa tamko kuwa Serikali iko mbioni kuanzisha chuo maalum kwa ajili ya kutoa mafunzo ya ufugaji bora wa nyuki ikiwa ni lengo la kuhakikisha sekta ya misitu na nyuki inakuwa kwa kasi na kuweza kumletea tija mwananchi.
Hata hivyo ili Serikali iweze kufikia malengo hayo ni vyema ikahakikisha maofisa ugani wanawafikia wananchi katika maeneo ya vijijini kwani ndiko kuliko na wananchi wengi ambao bado hawana uelewa mkubwa juu ya ufugaji wa nyuki jambo ambalo linawapelekea baadhi yao kujikuta wakiharibu mazingira huku baadhi yao wakikumbwa na ulipaji wa fidia kutokana na uharibifu huo

No comments:

Post a Comment