30 September 2013

TOZO ZA LAINI: WAMILIKI SIMU KUKATWA 3,00/-

  • KUANZIA JULAI MWAKA HUU,TRA YATOA SIKU 14
  • WATEJA WENGI KUKOSA MAWASILIANO HASA VIJIJINI


 Na Mwandishi Wetu

  Kilio cha Watanzania wengi kutaka tozo ya sh. 1,000 kila mwezi kwa laini moja ya simu ifutwe, bado kipo mashakani baada ya Mamlaka ya Mapato nchini (TRA), kuzitaka kampuni za simu nchini kulipa tozo hiyo kuanzia Julai mwaka huu ndani ya siku 14.


 Awali tozo hiyo ilitakiwa kuanza kulipwa Julai mwaka huu, lakini kutokana na malalamiko ya wadau, utekelezwaji huo ulisubiri mapendekezo ya Tume Maalumu iliyoundwa na Rais Jakaya Kikwete kushughulikia tatizo hilo.

 Hivi karibuni, Umoja wa Wamiliki wa Kampuni za Simu nchini (MOAT) ulisema asilimia 48 ya Watanzania ndio wanaotumia simu za mkononi sawa na watu milioni 22.Kutokana na tozo hiyo, zaidi ya asilimia 40 hadi 45 watafungiwa simu zao na kudai takribani Watanzania milioni nane, hushindwa kuweka sh. 1,000 kwa mwezi katika laini za simu zao.

MOAT waliongeza kuwa, kuendelea kukua kwa sekta ya mawasiliano hasa maeneo ya vijijini, kutakuwa na mashaka kwani wengi wao watashindwa kumudu gharama za simu hivyo kukwamisha malengo ya Umoja wa Kimataifa katika maendeleo ya mawasiliano. Tume iliyoundwa na Rais Kikwete ilijumuisha wajumbe kutoka TRA, Wizara ya fedha na wawakilishi wa kampuni za simu

 Julai 19 mwaka huu, Waziri wa Fedha, Dkt. William Mgimwa, alisema Serikali imekubali kupitia mawazo na maoni ya MOAT kuhusu kufutwa kwa tozo hiyo ambayo imelalamikiwa na wadau wengi wa sekta ya mawasiliano.

Hali hiyo ilitokana na kauli za baadhi ya viongozi wa Serikali, wabunge na wananchi wanaopinga tozo hiyo wakidai huo ni mzigo kwa watumiaji simu hasa wa kipato cha chini.

Dkt. Mgimwa alisema walikutana na MOAT na kupokea mapendekezo yao ambayo wanayafanyia kazi ili tupunguze makali ya kodi hiyo kwa wananchi wa hali ya chini. Alionya kusiwepo na jazba kwani suala hilo ni la kisheria kwa sababu lilipitishwa bungeni hivyo ili kuondolewa lazima ufuatwe utaratibu kwani hakuna mtu anayelenga kumkamua mwananchi.

  Alisema kodi hiyo ilitokana na mapendekezo 67 yaliyotolewa na Kamati ya Bajeti kuwa chanzo cha mapato kinachotekelezeka lakini kama inaonekana kikwazo, wataliangalia jinsi ya kukabiliana nalo

 Aliongeza kuwa lengo la tozo hiyo ni kupata fedha ambazo zitaelekezwa katika miradi ya maji, barabara na umeme hasa vijijini ambako kuna changamoto nyingi za maendeleo.

Alisisitiza kuwa, hakuna mtumiaji wa simu ambaye ameanza kukatwa tozo hiyo kutokana na mchakato huo kuwa bado unaendelea katika utekelezaji wake

 Naye Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Profesa Makame Mbarawa, alisema Serikali itahakikisha mwananchi hapati mzigo usiokuwa na sababu.

Aliongeza kuwa, Serikali ni sikivu na inawasikiliza wananchi wake, hivyo kupitia mawazo na mapendekezo mbalimbali yaliyotolewa, yatafanyiwa kazi ili kutokuathiri pande zote.
 

No comments:

Post a Comment