05 September 2013

SIMANZI ZATAWALA KESI YA MSUYA



Na Martha Fataely, Moshi
HALI ya taharuki na simanzi jana vilitawala katika Mahakama ya Kakimu mkazi mjini Moshi wakati wa kesi ya watuhumiwa wa mauaji ya mfanyabiashara wa Arusha, Erasto Msuya baada ya ndugu wa marehemu kuangua vilio na wengine kupoteza fahamu kwa muda.

Tukio hilo linafuatia wanandugu hao kuwaona washtakiwa katika kesi hiyo ambayo iliahirishwa hadi Septemba 18, mwaka huu kutokana na kutokamilika kwa upelelezi wake.Wanandugu ambao ni dada wa marehemu Msuya, Antuja Msuya na Bahati Msuya, ambao waliangua vilio huku wakidai kaka yao ameuawa kikatili pia walianguka chini na kupoteza fahamu ingawa waliondolewa na kupelekwa katika magari ya ndugu wengine waliokuwepo.
Pamoja na hilo lakini pia Jeshi la Polisi kutokana na umati wa wakazi wa manispaa hiyo walifurika mahakamani hapo, liliimarisha ulinzi kwa kutumia askari kanzu, wale wa kutuliza ghasia (FFU), askari wa pikipiki na kikosi maalum cha kupambana na majambazi wote wakiwa na silaha.
Awali mbele ya Hakimu Mkazi wa mahakama hiyo, Theotimus Swai,wakili wa Serikali, Stella Majaliwa aliieleza mahakama kuwa mshtakiwa wa pili, Shaibu Mpungi hakufika mahakamani hapo kutokana na kusumbuliwa na maradhi ingawa hakuyabainisha.Wakili Majaliwa aliieleza mahakama hiyo kuwa anaomba kuahirishwa kwa kesi hiyo kutokana na kutokamilika kwa upelelezi wa shauri hilo.
Naye wakili wa utetezi anayewatetea mshtakiwa wa kwanza Sharifu Mohamed na wa tatu Musa Mangu, aliuomba upande wa mashtaka kuharakisha upelelezi ili kuanza kusikilizwa kwa kesi hiyo mapema.Akiahirisha kesi hiyo,hakimu mkazi wa mahakama hiyo, Swai alisema maombi ya upande wa utetezi yamesikika na upande wa mashtaka na hivyo kutaka washtakiwa hao kurudi rumande hadi Septemba 18, mwaka huu.
Kesi hiyo ilifikishwa mahakamani hapo Agosti 21 mwaka huu, ambapo watuhumiwa hao wanakabiliwa na mashtaka ya kuua kwa kukusudia mfanyabiashara wa madini, Msuya kwa kumpiga risasi.Mfanyabiashara huyo aliuawa Agosti 7 mwaka huu saa 6:30 mchana kwa kupigwa risasi 13 kifuani, kando ya barabara kuu ya Arusha - Moshi katika eneo la Mjohoroni, Wilaya ya Hai, karibu na Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA).

No comments:

Post a Comment