05 September 2013

MWINYI AZINDUA KIPIMO KIPYA CHA MALARIA



Na Salim Nyomolelo
WAZIRI wa Afya Dkt. H u s s e i n M w i n y i amezindua kipimo cha malaria kinachotoa majibu ya haraka (mRDT) katika vituo binafsi vya kutolea huduma za afya huku akisisitiza wananchi kupima kabla ya kumeza dawa.

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana mara baada ya kuzindua kipimo hicho Dkt. Mwinyi alisema kuwa asilimia 40 ya Watanzania wanatibiwa katika vituo binafsi vya kutolea huduma za afya na hivyo ni vyema kipimo hicho kikatumika pamoja na vituo hivyo.
Alisema kuwa mRDT itasaidia kutoa majibu ya haraka na kuthibitisha kama mgonjwa ana ugonjwa wa malaria kwa vituo ambavyo havina huduma za maabara.Alisema kuwa utafiti katika jamii kwa muda wa miaka mitano unaonesha kuwa maambukizo ya ugonjwa wa malaria yamepungua kwa zaidi ya asilimia 50 kutoka asilimia 18 mwaka 2007 hadi kufikia asilimia 9 mwaka jana.
“Kutokana na kazi nzuri ya kupambana na ugonjwa wa malaria, tumepata mafanikio makubwa na kiasi cha maambukizo kimepungua na wizara inasisitiza kutumia mkakati mpya wa kupima kabla ya kutumia dawa na kujua ni ugonjwa gani unakusumbua,” alisema Dkt. Mwinyi
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Tiba Wizara ya Afya, Magreth Mhando alisema kuwa mRTD ni kipimo cha haraka cha kutambua malaria na cha kuaminika ambapo kinatoa majibu kuanzia dakika 15 hadi 20 ya kuwepo ama kutokuwepo kwa vimelea vya malaria.Hata hivyo Mhando alisema kuwa alama ya kipimo hicho ni nembo ya V ya rangi ya bluu na vinapatikana kwa bei nafuu.

No comments:

Post a Comment