21 September 2013

OPERESHENI KIMBUNGA YAIBUA MAPYA


Na Mwandishi Wetu
  Operesheni Kimbunga ya kuwaondoa wahamiaji haramu nchini imezidi kuibua mambo mapya kutokana na kukamatwa kwa watuhumiwa wa ujambazi wa kutumia silaha 55, mabomu ya kurusha kwa mkono manane, bunduki 47
. Taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari jana Kiongozi wa Timu ya Habari na Mawasiliano ya Operesheni Kimbunga, Zamaradi Kawawa, juzi ilieleza kuwa watuhumiwa hao wamekamatwa kuanzia Septemba 6, 2013 hadi kufikia Septemba 17, 2013.
Alisema miongoni mwa silaha zilizokamatwa katika operesheni hiyo ni bunduki aina ya SMG (4) Shotgun (4) Riffle (2) Mark IV (1) na Gobori 37.Alisema risasi 602 zilikamatwa zikiwemo risasi 500 za bunduki ya aina ya SMG na SAR, risasi (20) za bunduki aina ya Mark IV na risasi (82) za bunduki aina ya Gobori, fataki (8), mitambo ya kutengeneza magobori (2), misumeno ya kukata miti (9), mbao (1,516), magogo (86), na mkaa magunia (111).
  Kwa mujibu wa taarifa hiyo tangu kuanza kwa Operesheni hiyo ya kuwaondoa kwa lazima imefanikiwa kuwahamisha nchini wahamiaji haramu 7,819.Aliongeza kuwa watendaji wa Operesheni Kimbunga pia wamefanikiwa kukamata majangili Watanzania watatu, vipande vya meno ya tembo (2), pamoja na ngozi za wanyama mbalimbali..
  Wakati huo huo, ng'ombe 3,436 wamekamatwa baada ya wafugaji haramu kutelekeza mifugo hiyo wakati walipozingirwa na timu ya operesheni kimbunga katika mikoa ya Kagera, Kigoma na Geita."Kumekuwepo na tabia ya baadhi ya wamiliki wa mifugo kutoka nchi jirani ambao wengi wao ni matajiri na viongozi Serikalini kuwatuma watumishi wao kuingiza mifugo katika ardhi ya Tanzania hususan kwenye hifadhi ya Taifa kwa ajili ya malisho na watumishi hao hupewa silaha kwa ajili ya kujihami wakiwa kazini," alisema Zamaradi na kuongeza;
  "Operesheni Kimbunga itahakikisha inawakamata wahalifu wote wanaotishia amani hususan katika mikoa ya Kagera, Kigoma na Geita."Alisema wananchi ambao ni raia pamoja na raia wenye asili ya nchi jirani wanaowakaribisha na kuwahifadhi wahalifu na wahamiaji haramu watakamatwa na kufikishwa kwenye vyombo vya sheria.
  Operesheni Kimbunga inayoongozwa na Brigedia Jenerali Mathew Sukambi imeanza rasmi Septemba 6, 2013 baada ya kutoa muda wa wiki mbili kwa wahamiaji wanaoishi nchini bila kufuata sheria kuondoka kwa hiari.


No comments:

Post a Comment